Subscribe:

Ads 468x60px

Tunaalani vikali waandishi wa habari kupopolewa kwa mawe



Na Editor
20th August 2015
Katuni.
 
Katika toleo letu la jana ukurasa wa pili, kulikuwa na habari yenye kichwa cha habari `Waandishi wa habari wapigwa mawe.’

Tukio hili la wanahabari kupopolewa kwa mawe, liliripotiwa kutokea  katika kijiji cha Ruanda kata ya Ruanda Wilaya ya Mbinga mkoani  Ruvuma Agosti 17, mwaka huu ambako walikwenda kutekeleza majukumu yao ya kazi.
Imeelezwa kwamba baada ya kufika katika kijiji hicho, kundi la watu waliokadiriwa kufikia 40, walianza kuwashambulia wanahabari hao kwa mawe.

Katika tukio hilo, Mwenyekiti wa kijiji hicho cha Ruanda, Deogratias Haule, aliyekuwa amefuatana na wanahabari hao, pia alishambuliwa kwa mawe na kumsababishia majeraha puani na mdomoni na kupelekwa katika Hospitali ya Wilaya ya Mbinga kwa matibabu.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Ruvuma, Mihayo Msikhela, alithibitisha kutokea kwa tukio hilo lililotokea majira ya mchana.

Kamanda Msikhela aliwataja waandishi wa habari waliokumbwa na mkasa huo kuwa ni Kassian Nyandindi, wa magazeti ya kampuni ya Business Times, Aden Mbelle na Pastory Mfaume, kutoka Redio  Jogoo FM ya mjini Songea mkoani Ruvuma.

Alisema wanahabari hao walipatwa na mkasa huo baada ya kwenda kutekeleza majukumu yao ya kikazi ya kuandika tukio la kufungwa kufuli ofisi za kata ya Ruanda, kitendo kilichofanywa na baadhi ya wanakijiji hicho wasiofahamika.

 Kamanda Msikhela alisema baada ya wanahabari hao kukamilisha shughuli yao iliyowapeleka, ghafla liliibuka kundi la watu hao na kuanza kuwashambulia kwa mawe wakati wakijiandaa kurejea mjini Songea ambapo mmoja wa waandishi hao, alirushiwa jiwe usoni. 

Tukio hili siyo tu limetusikitisha sisi wanataaluma ya habari, bali pia limetushtua na kujiuliza maswali mengi yasiyo na majibu.

Tunasema ni tukio la kinyama na lililokosa hata chembe ya ustaarabu.

Hatujui waliofanya unyama huu kama wana malengo gani, lakini kwa vyovyote vile, kitendo hiki kinapaswa kulaaniwa vikali na kila mpenda amani.

Tunaliomba Jeshi la Polisi mkoani Ruvuma lifanye uchunguzi wa kina kuwabaini wote walioshiriki kufanya uhalifu huu na sheria ichukue mkondo wake.

Aidha, tunalipongeza pia Jeshi la Polisi mkoani Ruvuma kwa kumshikilia mtuhumiwa mmoja kuhusiana na tukio hili katika hatua hizi za awali tukiamini kwamba juhudi zaidi zitafanyika kuhakikisha kwamba wote walioshiriki kwa namna moja ama nyingine, wanapatikana na kufikishwa mbele ya vyombo vya sheria.

Tunaamini kwamba jamii inafahamu fika mchango wa wanahabari katika kulisukuma mbele gurudumu la maendeleo la Taifa letu isipokuwa watu wachache kama hao waliowapiga wanahabari, wana lao jambo.

Tunasema tunaalani kwa nguvu zote kitendo hiki ambacho kwa hakika tunajiridhisha kuwa kimefanywa na wachache wenye upeo mdogo wa kuelewa majukumu ya wanahabari mbele ya jamii.
CHANZO: NIPASHE
http://www.ripoti.com/openx/www/delivery/lg.php?bannerid=647&campaignid=424&zoneid=267&loc=http%3A%2F%2Fwww.ippmedia.com%2F%3Fl%3D83478&referer=http%3A%2F%2Fwww.ippmedia.com%2F%3Fm%3D54%26lang%3DSW&cb=9a3d02a888

0 comments:

Post a Comment