Subscribe:

Ads 468x60px

Ukawa: Hatutakubali kujadili rasimu nyingine



Mjumbe wa Umoja wa Wanaotetea Katiba ya Wananchi (Ukawa), Profesa Ibrahim Lipumba akizungumza na waandishi mjini Dodoma jana, mara baada ya kujadili hotuba ya Rais Jakaya Kikwete aliyoitoa katika Bunge Maalumu la Katiba juzi. Kushoto ni Mjumbe wa Ukawa, Freeman Mbowe na kulia ni Tundu Lissu. Picha na Salim Shao 
Na Mussa Juma, Mwananchi

Posted  Jumapili,Marchi23  2014  saa 11:17 AM
Kwa ufupi
Alisema kauli za Rais badala ya kuimarisha umoja zimewagawa Watanzania kwani ametoa vitisho ambavyo havina sababu hasa kwa Wapemba bila kujua kuna Wanyamwezi wanaoishi Zanzibar.


Dodoma. Bunge Maalumu la Katiba sasa lipo katika hati hati ya kuendelea kutokana na viongozi wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), kutangaza kuwa hawatakuwa tayari kujadili rasimu tofauti na iliyowasilishwa na Jaji Joseph Warioba bungeni.
Wakizungumza katika mkutano na waandishi wa habari jana katika Ukumbi wa Pius Msekwa bungeni, viongozi wa Ukawa, Profesa Ibrahim Lipumba, James Mbatia, Freeman Mbowe na Tundu Lissu, walisema wataitetea rasimu hiyo, ndani ya Bunge na kwenye Kamati.
“Rais Jakaya Kikwete amekuja bungeni siyo kufungua Bunge la Katiba bali kaja na mapendekezo ya rasimu ya CCM, sisi tutajadili rasimu ya wananchi ya Jaji Joseph Warioba ambayo inazungumzia muundo wa Muungano wa Serikali tatu,” alisema Profesa Lipumba.
Kutokana na msimamo huu wa Ukawa huenda Bunge litakwama kwani kwa mapendekezo ya CCM yenye Muundo wa Muungano wa Serikali mbili ni lazima kuandikwa upya Rasimu ya Katiba au kufanyika mabadiliko makubwa.
Profesa Lipumba alisema katika majadiliano juu ya rasimu, Ukawa watajikita kutumia Rasimu ya Katiba waliyopewa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba, ambayo imeeleza mapendekezo kwa nini yamefikiwa katika kila hoja,” alisema.
Hata hivyo, alisema wamesikitishwa sana na Rais Jakaya Kikwete, badala ya kufungua Bunge alijikita katika kuchambua rasimu na kuikosoa tume aliyoiunda mwenyewe.
“Rais Jakaya Kikwete siyo tu amemdhalilisha Jaji Warioba pamoja na wajumbe wa Tume, bali amewadhalilisha wananchi waliotoa maoni kwani hata takwimu alizotoa za kupinga rasimu siyo za kweli,” alisema Profesa Lipumba.
Alisema muundo wa Serikali tatu ndio mawazo ya wananchi ambayo yamekusanywa na watu wenye heshma wakiwapo Jaji Warioba aliyewahi kuwa Waziri Mkuu na Makamu wa Rais na Jaji Augustino Ramadhani ambaye pia amewahi kuwa Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Jaji Mkuu wa Zanzibar.
Alisema kauli za Rais badala ya kuimarisha umoja zimewagawa Watanzania kwani ametoa vitisho ambavyo havina sababu hasa kwa Wapemba bila kujua kuna Wanyamwezi wanaoishi Zanzibar.
Mbatia
Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, James Mbatia ambaye pia ni mjumbe wa Bunge hilo, alisema kwa kauli ya juzi ya Rais Kikwete, kutangaza kuwapatia Zanzibar; watu, ardhi, mamlaka kamili na kusimamia uhusiano wa kimataifa ni kuvunja rasmi Muungano,
Mbatia alisema Rais Kikwete pia amewagawa Watanzania katika kauli zake ikiwa ni pamoja na ile ya Wapemba kwa kulima vitunguu katika Jimbo la Kibakwe kana kwamba ni makosa.


Alisema wamesikitishwa na Rais kuacha kufungua Bunge badala yake katumia taarifa potofu za mitaani kuligawa Bunge na kuwadhalilisha wajumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba.
“Hakuna asiyejua sasa tupo katika mgogoro mkubwa wa kikatiba, Zanzibar tayari ni nchi kamili kutokana na mabadiliko ya 10 ya katiba yao waliyoyafanya mwaka 2010 baada ya kupitisha dhana ya kuwa Zanzibar ni nchi,” alisema.
Mbowe
Mbowe alisema Rais amevunja maridhiano na hata kushindwa kusikiliza maoni ya aliyekuwa Mwanasheria Mkuu wa Kenya, Seneta Amos Wako kuwa maoni ya wananchi yaheshimiwe.
Alisema Serikali ya Kenya ilichakachua maoni, ilichakachua rasimu na kusababisha vurugu kubwa jambo ambalo linaweza kutokea kwa Tanzania.
“CCM wasijidanganye kwa wingi wao bungeni hakika katika hili tutatetea madai na maoni ya wananchi hadi mwisho,” alisema


Kitaifa Warioba:‘Tumemaliza kazi yetu’

Jaji Joseph Warioba 
Na Editha Majura, Mwananchi

Posted  Jumapili,Marchi23  2014  saa 11:8 AM
Kwa ufupi
Mjumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Profesa Mwesiga Baregu alisema alitarajia Rais Kikwete angezindua Bunge Maalumu na siyo kutoa maagizo na vitisho kwa wajumbe.



Dodoma. Siku moja baada ya Rais Jakaya Kikwete kuzindua Bunge na kuponda ripoti ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Mwenyekiti wa Tume hiyo Jaji Joseph Warioba amesema jukumu walilopewa kwa mujibu wa sheria wamelikamilisha na wanawaachia wananchi waamue.
Akizungumza na Mwananchi jana asubuhi, Jaji Warioba alisema alichokizungumza Rais Kikwete ni maoni yake na kwamba hawezi kuyajadili.
“Rais Kikwete alichozungumza ni maoni yake, kwa sasa sipendi kuyazungumzia hayo, ” Jaji Warioba alieleza.
Alisema wamemaliza jukumu walilopewa na kwamba sasa jukumu lote lipo mikononi mwa Bunge.
Jaji Warioba alisema Tume yake ilikusanya maoni kutoka kwa wananchi, mabaraza ya wilaya ya Katiba na Taasisi mbalimbali, wakatengeneza rasimu ambayo sasa wameikabidhi kwa Bunge Maalumu la Katiba.
Jaji Warioba pia alikataa kuzungumzia zogo lililoibuka bungeni na kusababisha rasimu kuwasilishwa Jumatano, baada ya kikao cha Jumanne kuvunjika.
Hali hiyo ilitokana na UKAWA kudai muda wa saa 1:30 uliokuwa umepangwa Jaji Warioba ahutubie bungeni uongezwe na kanuni inayoelekeza Rais Jakaya Kikwete ahutubie kabla Jaji Warioba hajawasilisha rasimu izingatiwe, baada ya kutangazwa kuwa Rais angehutubia baada ya rasimu kuwasilishwa.
Profesa Baregu
Mjumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Profesa Mwesiga Baregu alisema alitarajia Rais Kikwete angezindua Bunge Maalumu na siyo kutoa maagizo na vitisho kwa wajumbe.
Alisema hajui lengo la Rais kufanya alichofanya lakini ana hakika kwa kutoa ufafanuzi wa hoja zilizotokana na maoni ya wananchi ndani ya rasimu, ameingilia kazi za Tume na hivyo amevunja Sheria ya Mabadiliko ya Katiba (Sura ya 83 toleo la mwaka 2012), inayosema:
“21.-(b) atakayejifanya kuwa mjumbe wa Tume au Sekretarieti; au (c) atakayeendesha programu ya elimu juu ya mabadiliko ya katiba kinyume na masharti ya sheria hii, atakuwa ametenda kosa.
(3) atakayetiwa hatiani kwa kutenda kosa kinyume na Sheria hii, atawajibika kulipa faini isiyopungua Sh2,000,000 (milioni mbili) na isiyozidi Sh5,000,000 (milioni tano) au kifungo kwa muda usiopungua mwaka mmoja na usiozidi miaka mitatu au adhabu zote mbili.

Sheria hiyo inaendelea kuelekeza, (4) Hatua zozote zilizochukuliwa chini ya kifungu hiki hazitachukuliwa kuwa zimefikia ukomo na zitaendelea kuwa na nguvu ya kisheria hata baada ya Sheria hii kukoma kutumika.”
Profesa Baregu alisema sheria imezungumzia mtu yeyote, hajui kwa Rais inakuwaje.
“Sijui ameona Bunge halitoshi, haliwezi kung’amua mambo au limepungukiwa kiasi cha kushindwa kumudu majukumu yake? Sielewi ila amevunja sheria na amelivunjia Bunge hadhi yake kiasi kwamba hata kazi yake inaweza isiaminike,” alieleza.
Profesa Baregu alisema Rais Kikwete amejipa jukumu la kujibu na kujadili hoja za rasimu na hivyo kuwa sehemu ya Bunge Maalumu.
Alisema wakati wabunge wanahimizwa kutumia mfumo wa maafikiano katika kuamua mambo, Rais amewajengea msingi wa mgawanyiko na chuki, hali itakayoathiri mpango wa kulipatia taifa Katiba inayotokana na wananchi.
Profesa Baregu alitaja baadhi ya kauli za Rais Kikwete ambazo zinaweza kuathiri mchakato kuwa ni kujirudia kwa kauli; “Nyie ndiyo mnaotunga Katiba (Wabunge wa Bunge Maalumu) kazi imebaki kwenu.” na maelekezo kwamba serikali tatu zitapatikana, lakini labda baada ya yeye (Rais Kikwete) kuondoka madarakani.
Jaji Ramadhan
Jaji Ramadhani alisema wao Tume wamemaliza kazi yao na kwamba sasa wanawaachia wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba na wananchi waamue.
“Tumemaliza kazi yetu na sasa tunawaachia wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba na wananchi,” alisema.
Hata hivyo, alisema ikitokea wajumbe wa Bunge hilo wakihitaji ufafanuzi wa jambo lolote, yeye binafsi anaahidi kutoa ushirikiano.
Kuhusu hotuba ya Rais Kikwete bungeni juzi, alisema yeye alikuwa Arusha akishughulika na vikao vya Mahakama ya Kimataifa ya Haki za Binadamu na kwamba hakuwa amepata muda wa kuipitia na kuitafakari kwa kiwango cha kuizungumzia.
“Ninasoma na kuitazama kupitia vyombo vya habari na ninafahamu nyie wanahabari huwa mnalenga pale palipowakuna. Hivyo nikitulia na kupata hotuba halisi aliyotoa nikaitafakari; nitaizungumzia,” alieleza.
Rais Kikwete akizindua Bunge juzi mjini Dodoma, alisema rasimu ya pili iliyowasilishwa bungeni na Jaji Warioba ina makosa mengi ya kiuandishi.
Alisema ina mambo mengi, baadhi yalitakiwa kuwekwa kwenye Sheria.
“Mbolea, mbegu, pembejeo vyote vimewekwa humo, hata umri na haki ya mtoto kupewa jina vinawekwa humo, yakiwekwa yote kama yalivyo, serikali haitaweza kuyatekeleza itashtakiwa mahakamani kila wakati,” alieleza.
Rais Kikwete aliwataka wajumbe wa Bunge Maalumu kusoma neno kwa neno, mstari kwa mstari na kujiridhisha na mambo watakayoidhinisha yaingie kwenye Katiba itakayopendekezwa.
Alisema watakachoona kinafaa kurekebishwa, kuboreshwa au kufutwa wasisite kufanya hivyo kwa sababu inatakiwa Katiba bora, inayotekelezeka na ambayo haitalalamikiwa kiasi cha kulazimika kuibadilisha muda mfupi baada ya kupitishwa.
Huku akishangiliwa na baadhi ya wajumbe, alisema wakichagua Serikali tatu watatakiwa kuondoa mambo yote yanayoweza kukanganya utendaji wa Serikali za washirika na ile ya Muungano. Lakini wakichagua Serikali mbili, mengi yatatekelezeka.
Rais Kikwete alisema serikali zote mbili zimeamua kwa dhati kutumia fursa ya mchakato wa mabadiliko ya Katiba kutatua mambo matatu kati ya sita ambayo bado hayajatatuliwa kutoka kwenye orodha ya kero 31 za Muungano zilizoainishwa na Zanzibar.
 

Wako: Msipuuze maoni ya Wananchi



 
Mwanasheria Mkuu mstaafu wa Serikali ya Kenya, Seneta Amos Wako akizungumza jana, wakati wa Semina ya Bunge Maalumu la Katiba. Picha na Salim Shao 
Na Habel Chidawali na Editha Majura, Mwananchi

Posted  Ijumaa,Marchi21  2014  saa 9:11 AM
Kwa ufupi
  • Awataka Wajumbe wa Bunge la Katiba watunge Katiba inayotokana na maoni na matakwa ya wananchi ili kuepusha migogoro.
Dodoma. Mwanasheria Mkuu (AG) mstaafu wa Kenya, Amos Wako amewataka wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba kutokupuuza maoni ya wananchi katika kutunga Katiba ya nchi vinginevyo watazua mgogoro.
Wako, ambaye kwa sasa ni Seneta wa Busia ya Mashariki nchini Kenya, alitoa ushauri huo jana katika semina kwa wajumbe wa Bunge la Katiba kuhusu uzoefu wa namna nchi hiyo ilivyopitia misukosuko ya kuipata Katiba mpya.
Wako ambaye kwa miaka 21 alikuwa katika wadhifa wa AG, alisema matukio mengi yaliyosababisha Kenya kutokupata Katiba yao kwa wakati, yalitokana na kutokuwashirikisha wananchi moja kwa moja katika mchakato.
Katika hotuba yake iliyodumu kwa saa 2: 11, mwanasheria huyo aliyewahi kuwa Mwenyekiti wa Tume ya Katiba ya Kenya alionya pia kuwa Katiba inayotengenezwa hapa nchini isiwe ya kunukuu kutoka katika mataifa mengine kwa sababu mahitaji yanatofautiana kwa kila nchi.
“Katiba isiwe ya mazungumzo kutoka kwa viongozi pale Dar es Salaam, kwani itakuwa ni mali ya watu wachache na ambayo lazima itapingwa, hata sisi tulianza hivyo lakini tulishindwa vibaya,” alionya Wako.
Aliimwagia sifa Rasimu ya Katiba iliyowasilishwa bungeni Jumanne iliyopita, kwamba kwa mtindo ilivyowasilishwa inaonekana kuwajali na kuwapa nafasi zaidi wananchi wa hali ya chini.
“Pamoja na hayo, lakini Katiba hii ikiingiliwa zaidi na kutekwa na wanasiasa au kikundi cha watu wachache kwa masilahi yao, inaweza kuharibika kama ilivyotokea kwetu Kenya ambako Kanu walikuwa wakipinga kila kitu wakatufanya tuingie katika mgogoro.”
Alisema kuwa mitazamo ya wanasiasa huwa ni tatizo na hatari katika kutafuta Katiba mpya na dawa pekee na ya maana ni kutoa nafasi kwa wananchi waamue wenyewe.
“Mfumo uliowekwa katika mchakato wa kuunda Katiba mpya nchini kwenu, kwamba Rasimu ya mwisho ya Katiba itoke bungeni na kupelekwa moja kwa moja kwa wananchi ni mzuri, ni muhimu maoni ya wananchi ya awali yazingatiwe,” alisisitiza.
Kwa mujibu wa mwanasheria huyo, Bunge Maalumu limeaminika kufanya kazi hiyo ili kuwasaidia wananchi kufikia malengo yao.
Uzoefu wa Kenya
Akizungumzia uzoefu wa Kenya katika kupata Katiba mpya alisema walianza kwa kukabiliana na changamoto kubwa ya ukabila ambayo kila jamii ilikuwa haiamini kundi jingine katika kutafuta usawa, jambo alilosema ni tofauti na Tanzania.
  •  
SHARE THIS STORY
Related Stories
“Mwaka 1991 nilipoteuliwa kuwa Mwanasheria Mkuu, niliulizwa ningetaka nini zaidi ambacho nitawafanyia Wakenya, nikajibu kuwa ningependa kuwa na Katiba mpya yenye kutoa haki na uhuru wa kweli kwa Wakenya,”  alisema.
Alisimulia kisa chake kwamba kutokana na ahadi hiyo, alikwenda Uswisi ambako alijifungia peke yake chumbani na kuandika Rasimu ya Katiba ndani ya siku 10, kisha akarejea Kenya na kuwaambia alichokifanya lakini akakataliwa na wengi akiwamo aliyekuwa Rais wa Kenya, Daniel Arap Moi.
Alisema mwaka 1995, Rais Moi alitangaza kuteua kamati ya wataalamu watakaoandaa upatikanaji wa Katiba na katika mchakato huo  walialikwa wataalamu watatu kutoka Ufaransa, Uganda na Zambia.
“Changamoto tuliyoipata kwa wakati huo ni kwamba, tuliambiwa kuwa tusiposhirikisha vyama vya kijamii na taasisi nyingine, wataweza kuipindua Serikali, hapo nataka kuonyesha namna gani makundi ya kijamii yalivyo ya muhimu zaidi,” aliongeza.
Hofu ya Kanu
Alisema kuwa Kanu bado iliendelea kuwa na hofu juu ya uchaguzi kutokana na jinsi mambo yalivyoanza kuwa motomoto baada ya tangazo la kuingia katika mfumo wa vyama vingi mwaka 1992, lakini tofauti na matazamio yao, Rais Moi aliibuka na ushindi mkubwa.
Baada ya hatua hiyo, alisema wanasiasa kutoka katika chama hicho kilichokuwa madarakani walisema hakukuwa na haja ya kuwa na Katiba mpya, bali wafanye maboresho kidogo kitendo kilichoibua hisia kali kutoka vyama vya upinzani.
Kingine ni Kanu kukataa kuingiza uwiano katika uchaguzi wa wabunge kwa madai ya wingi wao katika Bunge, jambo lililopingwa na wengi na kusababisha kuunda umoja uliojulikana kama Ufungamano.
Mwafaka katika Katiba
Kuhusu mwafaka alisema ulifika wakati ambao kila Mkenya aliona ipo haja ya kuwa na Katiba bila ya kujali maeneo wala mazingira anayotoka, ndipo wakakubaliana kukaa pamoja katika eneo la Boma na wakati huu walishiriki wabunge wote na wajumbe watatu kutoka kila wilaya na suala la mgawanyo wa majimbo likaibuka.
Rasimu yakataliwa
Pamoja na mambo yote, kosa lilikuwa jinsi walivyoipitisha kwa AG (yeye mwenyewe) ambapo alitakiwa kurekebisha katika maeneo 13, kisha akaipeleka bungeni, jambo lililoibua hasira za watu wakaamua kuipinga kwa makusudi.
“Huo ulikuwa ni mvutano wa kuonyeshana mabavu kwa wanasiasa na makundi mengine, kikubwa kilikuwa katika muundo wa majimbo na mgawanyo wa madaraka katika kuzalisha majimbo, ili kuwepo na seneta na gavana kabla ya wabunge,” alisema.
Anasema kuwa mamlaka zinatakiwa kuanzia ngazi ya mwanzo hadi katika ngazi ya Taifa likiwemo suala la kuangalia mgawanyo wa mapato ili kuondoa manung’uniko.
Ushauri Katiba ya Tanzania
“Katiba Mpya ambayo inatakiwa ni ile ambayo inaihusisha jamii moja kwa moja, tume yenu imefanya kazi nzuri na mpangilio uliofanywa na Rais kutanguliza maoni ya wananchi na kisha wao kuwa wa mwisho kuamua ni mpango mzuri ambao hata mimi nimeupenda,” alisema Wako. Alirudia maneno kuwa lazima maoni na matakwa ya wananchi yaangaliwe kwa umakini mkubwa kabla ya kuwarudishia ambapo watakwenda kuamua kwa busara bila ya malumbano.
Maswali ya wabunge
Mbunge wa Kongwa, Job Ndugai alimuuliza Wako kuhusu namna walivyokubaliana katika kugatua madaraka na njia bora ya kugawana rasilimali na katika majibu yake, Wako alisema kinachoweza kuondoa malalamiko hayo ni uamuzi wa wananchi katika Katiba ambayo inakwenda kutungwa itakayoeleza namna ya kugawana rasilimali za nchi kwa usawa.
Profesa Abdallah Safari aliuliza kwa nini Wako alitumia lugha ya Kiingereza katika hotuba yake, huku akijua kuwa Katiba ya Kenya katika ibara ya 8 imetamka wazi kuwa Kiswahili ndiyo lugha ya taifa hilo.
Wako aliomba radhi kuwa bado hajakijua Kiswahili vizuri kutokana na mazoea, na akasema alipochaguliwa alikwenda Zanzibar kujifunza Kiswahili kwa mwezi mmoja huku akiwataka watu kutumia lugha hiyo inayokuwa kwa kasi barani Afrika.