Subscribe:

Ads 468x60px

askari Senapa waua jangili na kukamata bunduki smg AK47 risasi 258


ASKARI SENAPA WAUA JANGILI,WAKAMATA BUNDUKI SMG AK 47 ,RISASI 258.
Na Mwandishi wetu-Serengeti.
Novemba 30,2012.

ASKARI wa hifadhi ya Taifa ya Serengeti wamefanikiwa kumuua mtuhumiwa mmoja wa ujangili ,kukamata silaha ya kivita aina ya Smg AK 47,risasi258 , meno mawili ya tembo na msumeno wa kukatia meno ya tembo na shoka.

Tukio limethibitishwa na kamanda wa polisi mkoa wa Mara Absalom Mwakyoma linadaiwa kutokea novemba 29,majira ya saa 12;30 jioni katika eneo la Itaro ndani ya hifadhi ya Taifa ya Serengeti,eneo ambalo kumewekwa Faru waliotolewa Afrika Kusini,maarufu kama Faru wa JK.

Alisema aliyeuawa hajafamika ingawa anakisiwa kuwa na umri kati ya miaka 27,33 na kuwa katika majibizano hayo alipigwa risasi mguu wa kulia iliyopelekea kufa na wenzake wanakisiwa kuwa wanne kukimbia ,na hakuna aliyekamatwa kutokana na tukio hilo.

Habari za uhakika kutoka eneo la tukio zinadai kuwa askari wa hifadhi hiyo wakiwa doria walisikia milio ya bunduki na kufuatilia walikuta kundi kubwa la majangili wanaokadiriwa kufikia watano  wakiwa na silaha za kivita wameishaua tembo mmoja na wametoa meno.

“Walianza kutushambulia kwa risasi,kukatokea majibizano makali yaliyochukua muda ambayo yanaonyesha kuwa walikuwa na risasi za kutosha kwa kuwa walikuwa na silaha za kivita,mmoja akawa amepigwa risasi na kuanguka …wenzake walipoona hivyo wakakimbia mmoja akiwa na bunduki,”kulisema chanzo kimoja cha uhakika.


“Maiti hiyo imehifadhiwa katika chumba cha maiti hospitali teule ya Nyerere ddh,haijatambuliwa ,inaonekana si mtu wa maeneo haya hali ambayo inaonyesha ukubwa wa mtandao huo kutoka mikoa mbalimbali kwa kushirikiana na wenyeji wa maeneo,kasi yao kuingia inakwenda sambamba na uingizaji silaha kutoka mikoa iliyoko pembezoni mwa mipaka ya nchi jilani”kilisema chanzo hicho.

Mganga mkuu wa Hospitali hiyo dk,Kelvin Mwasha amethibitisha kupokelewa kwa mwili wa marehemu huyo”amefikishwa hapa usiku wa manane na ameletwa na askari polisi…hawajaja polisi kwa ajili ya uchunguzi,tunawasubiri maana hatuwezi kusema kilichosababisha kifo bila kufanya uchunguzi”alisema daktari.

Mtandao wa ujangili ambao umesambaa hifadhi za taifa ,mapori ya akiba na maeneo ya wazi unadaiwa kufadhiliwa na wafanya biashara wakubwa wa ndani na nje ya nchi ambao wanahusishwa kuwa na ushirikiano wa karibu na baadhi ya watendaji wa jeshi la polisi,mahakama,maliasili ,uhamiaji na ofisi za wanasheria wa serikali na Tra.

Uhusiano huo huwawezesha kusafirisha shehena za meno ya tembo kwa kupita mipakani,bandarini,na kupeleka nje ya nchi,kasi hiyo ikienda sambamba na uingizaji wa silaha za kivita kwa ajili ya kazi hiyo.

Wakati huo huo mtu mmoja ambaye hajatambuliwa aliuawa na wananchi baada ya kukutwa akiiba mabati kwenye jengo la mtu aliyejulikana kwa jina Jumanne Kagosi katika kijiji cha Kwangwa kata ya Kigera Manispaa ya Musoma.

Kamanda Mwakyoma amesema tukio hilo limetokea novemba 29,majira ya saa 10 jioni mwaka huu na kuwa wananchi waliamua kuchukua sheria mkononi na kumpiga hadi kufa ,na kuomba wananchi wasijichukulie sheria mkononi badala yake wafikishwe kwenye vyombo husika.

Mwisho.


matukio ya kukabidhi vitabu na vifaa vya sayansi vilivyotolewa na HAKI ELIMU

Haki Elimu kupitia kwa marafiki wa Elimu wilayani Serengeti wametoa vitabu na vivunge kwa ajili ya masomo ya sayansi kwa shule nne za msingi za Mbalibali,Tamkeri,Mugumu B na Kambarage,makabidhiano hayo yamefanyikia ukumbi wa Halmashauri ya wilaya na ofisa michezo wa wilaya Makoye Maige kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa halmashauri hiyo,picha zote kwa hisani ya Mayunga.blogspot.com






mwandishi avunjika mkono


 Dick Mohammed mpiga picha wa Star Tv mkoa wa Mara muda mfupi baada ya kufungwa POP mkono  uliovunjika  baada ya gari walilokuwa wakisafiria kutoka Musoma kwenda Mugumu  kikazi kunusurika kuanguka katika eneo la Mugeta wilayani Bunda kutokana na utelezi.katika safari hiyo walikuwa na mwandishi wa TBC 1 Emmanuel Amasi ambaye hakupata madhara.picha zote na Anthony Mayunga

Ukeketaji kuanza desemba 15,2012


 wakati tarehe ya kuanza ukeketaji wilayani serengeti ikitajwa kuwa ni desemba 15 mwaka huu siku moja tu baada ya shule za msingi kufungwa wanaharakati wanaendelea na kampeini zao za kupinga vitendo hivyo vya ukatili wa kijinsia,picha kwa hisani ya Mayunga.blogsspot.com
 
UKEKETAJI  KUANZA DESEMBA 15 BAADHI YA MAENEO.
Na Anthony Mayunga-Serengeti
Novemba 28,2012.

WAKATI wanaharakati wanazindua siku 16 za kupinga vitendo vya ukatili wa kijinsia ,wazee wa baadhi wa mila baadhi ya maeneo  wilaya ya Serengeti wamepanga kuanza ukeketaji na tohara kwa vijana wa kiume kuanza desemba 15 mwaka huu.

Uamzi wa wazee wa mila kwa baadhi ya maeneo ambao unafanywa kisiri siri imebainika kuwa itakuwa ni siku moja baada ya kufungwa kwa shule za msingi desemba 14,2012.

Habari za uhakika ambazo zimethibitishwa na baadhi ya wazee wa mila zinadai kuwa muda huo umepangwa ukizingatia tarehe ambazo ngariba wa vijana wa kiume atakuwa amemaliza kazi nchini Kenya.

“Ngariba wa kiume anatokea nchini Kenya ambako kwa sasa wanaendelea na kazi ya kutahili…kuanzia tarehe hizo atakuwa amemaliza na ndiyo maana wamepanga tarehe hizo…”alisema  mmoja wa wazee wa mila jina limehifadhiwa.

Aliliambia Mwananchi kuwa ngariba wa kike wapo vijijini lakini kwa mila na desturi  watoto wa kike hawawatangulii vijana wa kiume,hivyo kazi hiyo itafanyika kwa wakati mmoja hasa maeneo ya kata ya Kebancha bancha.

Akizungumzia tishio la serikali la kuwakamata watakaohusika na kukeketa  watoto wa kike ,alisema kuwa kuacha itakuwa kazi ngumu kwa kuwa mila na desturi itakuwa imepotea.

“Ili kutopoteza mila wanakata kidogo sana ili damu ionekane imevuja,kuacha kabisa ni vigumu haya mambo yatakwenda taratibu yaishe yenyewe kama ilivyokuwa kwa kutoga masikio”alibainisha.

Hata hivyo baadhi ya maeneo wazee wa  mila wakiulizwa msimamo wao kuhusu kuacha ukeketaji wamekuwa wakisukumia wanawake kuwa ndio wanashawishi watoto wa kike ,huku akina mama wakisema wenye sauti ni wazee wa mila kwa kuwa ndio wanaoheshimiwa na jamii.

“Kuna kusukumiana kwa wazee wa mila na akina mama … wazee wa mila wanasema akina mama wanachangia kuendelea kwa ukeketaji kwa kuwa huwadanganya watoto kuwa wanaenda kusalimia bibi zao …huko hukeketwa kwa aibu yao kwa jamii ni kubwa kuliko wanaume,”alisema.

Kwa mjibu wa tafiti mbalimbali zinaonyesha kuwa wanawake wananyanyapaliana sana kama  kuliko wanaume hasa mabinti zao wanapokuwa hawajakeketwa,hali ambayo pia huwaathiri watoto wa kike kutengwa na wenzao na wengine hutoroka kwenda kukeketwa.

Baadhi ya mashirika yanayotoa  elimu ya kupinga vitendo vya ukeketaji  kwa wilaya za Serengeti na Tarime hasa Jumuiya ya Kikristo Tanzania(CCT)wamesema kuwa wana uhakika wa kupokea watoto wengi watakao kimbia kukeketwa.

Mwisho.


BABA ABAKA MWANAE WA MIAKA 2.5 NA KUMUUMIZA VIBAYA.
Na Anthony Mayunga-Serengeti
Novemba 28,2012.

WAKATI wanaharakati wakipaza sauti za siku 16 za kupinga ukatili ,mkazi mmoja wa mtaa wa Sedeko kata ya Stendi kuu wilayani Serengeti John Nashon(25)amembaka mwanae wa miaka 2.5 na kumuumiza vibaya kisha akatoroka.

Tukio hilo ambalo limepokelewa kwa hisia tofauti na wakazi wa mji wa Mugumu linadaiwa kutokea novemba 26,majira ya saa 12.00 jioni mwaka huu katika mtaa huo na kuripotiwa kituo cha polisi Mugumu mjini.

Mama mzazi wa mtoto huyo akiongea na Mwananchi akiwa hospitali teule ya Nyerere ddh alikolazwa kitanda namba 8 wodi ya watoto ,alisema wakati unyama huo unatendeka alikuwa sokoni.

“Nilimwacha mwanangu na baba yake ambaye ni fundi wa magari gereji ya Mayala mjini hapa,kurudi kufika mlangoni mme wangu akanieleza niingie ndani haraka nimkande mtoto mwili mzima kwa maji baridi…nilikuwa sijui kinachoendelea”alisema na kuendelea

“Kuingia chumba cha kulala nikamkuta mtoto amelala kitandani,kumnyanyua damu zikamwagika mithili ya maji kutoka sehemu yake ya siri…kumwangalia nikakuta amechanika sehemu zake za siri”alisema.

Hali hiyo ilimpelekea kumwangukia mwanae na kuanza kulia kwa uchungu na alipotaka maelezo kwa mme wake alisema alimsukuma kwa bahati mbaya mwanae akaanguka kwenye kochi na kuchomwa na msumari sehemu zake za siri.

“Nilipomwambia tumpeleke hospitali akakataa tena akinitishia kunipiga kwa madai kuwa siri itafichuka…niligundua kumbe ndiye kafanya unyama huo,nilitoka kwa nguvu hadi kituo cha polisi na kupewa pf 3,nikimwacha hapo,lakini alikimbia na haijulikani alipo”alisema.

Hata hivyo alipomuuliza mwanae kilichomtokea akasema kuwa baba yake ndiye aliyemfanyia unyama,huku akishangaa kwa kitendo hicho kwenye ndoa yao iliyodumu kwa mwaka mmoja toka novemba 2011.

Mganga mkuu wa hospitali hiyo Dk.Kelvin Mwasha amekiri kumpokea mtoto huyo na kuwa amelazwa wodi la watoto ,kutokana na maumivu na kuvuja damu nyingi ililazimu kuongezewa damu.

“Sehemu zake za siri zilikutwa zimeharibiwa sana ,amepata huduma ikiwa ni pamoja na kuchukua sampuli za maji yaliyokuwa yanatoka ukeni kwa ajili ya vipimo …amekutwa yuko salama,lakini hili tukio si la kawaida linatakiwa kulaaniwa ,na ndiyo yanaifanya wilaya kuonekana na matukio ya ukatili”alisema.

Hivi karibuni katika uzinduzi wa siku 16 zakupinga ukatili kamanda wa polisi mkoa wa Mara Absalom Mwakyoma alisema kunaongezeko kubwa la matukio ya ukatili,ambapo kwa mwaka huu toka januari yameripotiwa matukio 201 ikiwa ni tofauti na mwaka 2011 matukio 148 yaliriripotiwa polisi.

Mwisho.

Bomba lililokuwa likitiririsha maji machafu yaliyochanganyika na kinyesi lakarabatiwa





BOMBA LILILOKUWA LIKITIRIRISHA MAJI MACHAFU YALIYOCHANGANYIKA NA KINYESI LAZIBWA.
Na Anthony Mayunga-Serengeti
Novemba 19,2012.

HATIMAYE mamlaka ya mji mdogo wa Mugumu wilayani Serengeti umeziba bomba lililokuwa likitiririsha maji machafu yaliyochanganyika na kinyesi kwenda kwenye makazi wa watu na sehemu za biashara mtaa wa sedeko.

Uzibaji wa bomba hilo umekuja siku chache tu baada ya gazeti la Mwananchi kuripoti tukio hilo ambalo limepigiwa kelele ikiwa ni pamoja na kuwasilishwa katika vikao vya baraza la madiwani bila ufumbuzi.

Baadhi ya wakazi wa mtaa wa Sedeco waliliambia gazeti hili kuwa siku moja baada ya taarifa kutolewa hukuikionyesha picha ya tatizo hatua ilichukuliwa haraka .

“Tunawashukuru sana waandishi wa habari maana tumeumia sana kwa muda mrefu,mbunge amekuja mara mbili kapuuzwa ,baraza la madiwani lilidanganywa lakini mmekuja hapa na kuandika na hatua zikachukuliwa huku wakilaumu kwa nini tunawaambia waandishi,watendaji hawa hawafai mpaka wasukumwe”alisema mmoja akina mama ntilie eneo hilo jina limehifadhiwa.

Hata hivyo wakazi wa mtaa huo na wafanyabiashara walimtupia lawama afisa afya wa mamlaka hiyo kuwa utendaji kazi wake ni mbaya kwa kuwa wanapompelekea malalamiko anawajibu vibaya.

“Hatujui nafasi hizi wanazipataje maana ofisa afya wa mamlaka hii hafai bomba liko mita kumi toka ofisi yake ,tunamweleza anatujibu kuwa ,harufu hiyo inawapunguzia bajeti ya kula kwa kuwa matumbo yatashida yamejaa,tutegemee nini kwa mtumishi kama huyo analipwa kwa kazi gani”alihoji Phinias Edward mfanyabiashara wa chakula eneo hilo.

Hata hivyo alipotafutwa kwa njia ya simu afisa afya huyo Chironge Hamisi kutaka kujua utekelezaji wa kazi hiyo na malalamiko ya wananchi aling’aka.
“Wewe walikuletea malalamiko ili tutengeneze hilo bomba,kwanza wewe unaniuliza hayo wewe ni mkuu wangu wa kazi,mbona unaniuliza uliza haya mambo unataka nini,wewe nini bwana”alijibu kwa ukali na kukata simu.

Hata hivyo ofisa mtendaji wa mamlaka hiyo Gidioni Obel alidai kuwa matatizo yote hayo yanashughulikiwa kwa awamu na kuwa suala la bomba wamemaliza ,lakini ukarabati wa choo ikiwa ni pamoja na kuweka mifumo ya maji kwa kuwa ilijengwa vibaya inahitaji bajeti kubwa na wakipata fedha wataitekeleza.

Malalamiko ya wananchi wakiwemo wafanyabiashara ndani ya soko yalikuwa ni utiririshaji wa maji machafu yaliyochanganyika na kinyesi kwenye maeneo yao,huku baadhi ya wafanyabiashara wakilalamikia harufu mbaya inayotokana na choo  hicho kutokuwa na mfumo wa kutolea hewa na maji .

Mwisho.

Njaa yawatesa wakazi wa Ngorongoro


SERIKALI YALAUMIWA KWA KUTOPELEKA CHAKULA NGORONGORO LICHA YA KULIPWA.
Na Anthony Mayunga-Ngorongoro
November 18,2012.

SERIKALI imeombwa kuchukua za hatari kupeleka chakula kwa wakazi wa kata 7 zilizoko tarafa ya Ngorongoro wilayani Ngorongoro wanaokabiliwa na baa la njaa.

Wakazi wa tarafa hiyo iliyo ndani ya mamlaka ya hifadhi ya Ngorongoro hawaruhusiwi kulima kwa kuwa eneo hilo limehifadhiwa,na wanategemea shughuli za ufugaji ambazo zinakabiliwa na tatizo kubwa la ukame.

Mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya hiyo Elias Ngorika ameliambia Mwananchi kuwa hali ya chakula ni mbaya sana hali ambayo inatishia maisha ya wakazi wa tarafa hiyo kama juhudi za haraka hazitachukuliwa.

“Hali ni mbaya maana kilio hiki tumeishaiambia serikali inatakiwa kuzinduka… chakula kiliagizwa kwenye ghala la akiba ya chakula toka agosti fedha zimelipwa… hawajaleta,serikali isisubiri watu wafe ndipo izinduke “alisema kwa unyonge.

Alisema kiasi cha tsh,mil,315 zilizotokana na fedha zinazotolewa na mamlaka ya hifadhi ya Ngoro ngoro kwa baraza la wafugaji zimeishalipwa kwa ajili ya kupata tani 190 ,”chakula hicho kingepatikana hali ingekuwa nafuu”alisema.

Hata hivyo alisema kwa watu wazima kusubiri kupewa chakula kila wakati ni tatizo hivyo kungeangaliwa mfumo mwingine wa kuziwesha kiuchumi  familia zinazoishi ndani ya eneo hilo lililohifadhiwa .

Alisema baraza la madiwani katika kikao chacha hivi karibu waliamua kumwona Rais Jakaya Kikwete Arusha kumpelekea kilio cha wananchi ,lakini walizuia kukutana naye na kulazimika kukutana na mkuu wa mkoa.

“Kwa sasa suala hilo tumeliwekea mkakati wa kimkoa ili kuhakikisha tunawanusuru na vifo na magonjwa ya utapiamlo… hili suala lina uzito wake kwa kuwa wananchi hawatakuwa rafiki wa uhifadhi ili tusifike hatua mbaya wasaidiwe”alibainisha  Ngorika.

Mkakati wa kwanza kwa sasa wameunda kikundi maalum kinachoshirikisha wataalam ngazi ya mkoa ,wilaya na baadhi ya madiwani ili kujua ukubwa wa tatizo na taarifa itatoka ndani ya muda mfupi.

Kata ambazo zinakabiliwa na njaa ni Kakesio,Orbal orbal,Ngorongoro,Endulen,Nainokenoke,Naiyobi na Kapenjoro.

Afisa utawala baraza la wafugaji Ngorongoro Nakuroy Parkepu alisema serikali inatakiwa kuchukua hatua za kuwapa wananchi chakula kwa kuwa toka baraza limeagiza ni miezi mitatu lakini serikali haijawafikishia chakula.

“Hili ni tatizo la serikali sisi tumelipa toka agosti hawajaleta chakula wananchi wanahali mbaya …huu ni udhaifu wa serikali na vyombo vyake…hatuwezi kukiuka sheria za manunuzi “amebainisha.

Amekiri kuwa kila mwaka wa fedha mamlaka ya fifadhi Ngorongoro inatoa zaidi ya tsh,bil 1 kwa baraza kwa ajili ya shughuli za maendeleo,lakini zaidi ya tsh,mil 400 huelekezwa kwenye elimu,bado ujenzi wa sekondari ,afya ,maji na huduma zingine .

“Fedha hizo si za kununulia chakula,bali ni za huduma ya jamii,inapotokea tatizo kama hilo tunatoa hapo hapo ni kiasi kidogo”alidai.

Bei ya mahindi kwa sasa gunia moja ni tsh,78,000= ambayo wanategemea kutoka Karatu ambako kwa sasa debe ni tsh,12,000= kabla ya kusafirisha.

Makamu wa Rais wa jukwaa la Wanataaluma na Sauti ya Jamii wilayani Ngorongoro Onesmo Ole Ngurumwa akiongea na mwananchi kwa njia ya simu amesema serikali isikwepe lawama matatizo ya njaa kwa wakazi wa tarafa hiyo kwa kuwa imeshindwa kupeleka chakula kwa wakati.

“Jukwaa limeitisha kikao novemba 24 mwaka huu ili kuzungumzia hali hiyo na mengine ikiwemo mapigano,lakini haiwezekani watu waishi kwa chakula cha msaada  kila mwaka… huu ni udhaifu wa viongozi kufikiri”alibainisha.

Alikwenda mbali zaidi na kudai kuwa wilaya hiyo ni tajiri  ambayo inaingizia taifa takriban zaidi ya bilioni 50 kwa utalii ,wananchi wanaendelea kutaabika kwa kuishi maisha mabaya zaidinya wanyama .

Mwisho.