Subscribe:

Ads 468x60px

MAGEREZA WALIOKAMATWA NA TWIGA WATIMULIWA KAZI



JESHI la Magereza nchini limewafukuza kazi askari watatu na kumsimamisha kazi afisa wake mmoja kwa tuhuma za kukutwa na nyara za serikali kinyume cha sheria.
Mbali na hatua hiyo pia Mkuu wa gereza la Kiteto, Mrakibu wa Magereza Ally Sauko, amevuliwa madaraka na kurejeshwa katika Ofisi ya Mkuu wa Magereza Mkoa wa Manyara akisubiri hatua ya mamalaka ya kinidhamu dhidi yake kwa kutumia madaraka vibaya.
Askari waliofukuzwa kazi ni Sajenti Ketto Ramadhan, Koplo Silvester Dionice na Wada Barik huku afisa aliyesimamishwa kazi ni Joseph Kimaro ambaye ni mrakibu Msaidizi wa Magereza akifunguliwa mashtaka ya kinidhamu.
Taarifa ya jeshi hilo kwa vyombo vya habari ilieleza kuwa uchunguzi wa awali ulibaini ukiukwaji wa taratibu na maadili ya jeshi la Magereza na kwamba askari hao watapelekwa mahakamani baada ya upelelezi wa Polisi kukamilika .
Askari hao kwa kushirikiana na baadhi ya wananchi wanadaiwa kukamatwa na askari wa Kikosi cha Kuzuia Ujangili Kanda ya Kati Julai 23 mwaka huu wakiwa na nyara za serikali zenye thamani ya sh milioni 55.
Inadaiwa askari hao wakiwa na gari la magereza Toyota Land Cruiser lenye namba za usajili STK 4394 walikamatwa wakiwa wamepakia Twiga wawili, Majike mawili ya Swala Palapala na mbuni wawili.
Watuhumiwa walipopekuliwa katika gari walikutwa na kibali kilichoombwa na Hassan Omari kikiwaruhusu kuwinda nyati mmoja na pundamilia wawili.
Katika tukio hilo watuhumiwa wengine waliokamatwa ni Abubakari Ngaula, Hamza Ndachi, Saidi Idd na Husein Gola ambao pia walikutwa na bunduki ya aina ya SR mali ya Jeshi la Magereza pamoja na Rifle moja.