Subscribe:

Ads 468x60px

KUFUTWA KWA MATOKEO YA WATOTO 111 SEKONDARI MANCHIRA WAZAZI WAUNDA KAMATI KUFUATILIA



KUFUTWA KWA MATOKEO YA WATOTO 111 SEKONDARI MANCHIRA WAZAZI WAUNDA KAMATI KUFUATILIA .
Machi 13,2013
SERENGETI.

WAZAZI  wa watoto waliokuwa wanafunzi wa Manchira Sekondari wilayani Serengeti waliofutiwa matokeo kwa madai kuwa majibu yalikuwa ya mfanano wameibuka na kulitaka baraza la mitihani kupitia upya uamzi wake.

Wanafunzi 111  kati ya 114 waliohitimu kidato cha nne mwaka jana katika shule hiyo wamefutiwa matokeo na baraza la mitihani,taarifa ambayo inakinzana na ya awali kuwa majibu yao hayakutolewa kwa sababu hawakuwa wamelipa fedha ya mitihani.

Kutokana na utata huo wazazi wamelazimika kuunda kamati kwa ajili ya kufuatilia ili kujua ukweli wa taarifa ipi ni sahihi kwa kuwa awali wazazi waliambiwa hawakulipa fedha ya mitihani ingawa baadhi walikiri kulipa na mkuu wa shule hakuweza kutoa risti na anasakwa na polisi.

Katika barua hiyo iliyosainiwa na wajumbe 7 chini ya Mwenyekiti wao Daniel Washa inashangazwa na baraza la mitihani ambalo lilituma barua kwa mkuu wa shule ikibainisha kuwa matokeo yamezuiliwa kwa kuwa watoto hawakulipia mitihani.

“Taarifa ilitolewa januari 25,2013 kuwa baraza limetoa barua ya maelezo hayo,februari 21 katika kikao cha wazazi walikubali kulipa sh,35,000 kwa kila mzazi  …februari 22 tukawa tumekusanya sh,3,080,000 zikatumwa baraza la mitihani kupitia akaunti Na.2011100238 NMB na baada ya kupokea pesa machi 1 mkuu wa shule alidai alipokea  barua  ambayo inaonekana ilikuwa imeandaliwa mapema kuwa wamefutiwa majibu”imesema barua.

Wazazi hao wanahoji taarifa ya baraza la mitihani kuwa oktoba 9,2012 watahiniwa wakifanya mtihani wa Kiswahili msimamizi alikuta Toilet Paper yenye “Notes”za somo la Kiswahili kwenye dawati la mtahiniwa S3684/0003 na S3684/0072/0098/0105 na 0111 walikutwa na karatasi zenye notes za somo la Biology ndani ya chumba cha mtihani,lakini hawakuchukuliwa hatua kama wakosaji.

“Kwa kuwa watahiniwa waliofutiwa walikuwa vyumba vitatu tofauti ,je toilet paper zingeweza kuathiri vyumba vyote?,kama vyanzo vya baraza vimetaja majibu kufanana kwa masomo ya Physics,Biology na Chemistry ,iweje Kiswahili somo walilokutwa na Notes halikuhusishwa”wamehoji.

Kamati hiyo inayoundwa na Daniel Washa Mwenyekiti,Paulo Mtatiro Chacha(katibu)na wajumbe Simioni Nyatutu,Edina Mahemba,Damiani Thobias,Japhet Maduhu na Samwel Omar wamebainisha kuwa shule zilizofutiwa matokeo hutajwa kupitia vyombo vya habari lakini baraza liliomba watume fedha watoe matokeo na baada ya kufanya hivyo wakadai matokeo yamefutwa.

Na kuwa Baraza la Mitihani halikuhusisha ngazi ya wilaya husika kuhusiana na matokeo hayo ili kubaini udanganyifu huo badala yake limeibuka na majibu ambayo yameacha mashaka kwa kuwa walitaka malipo,wazazi wanahoji uhalali wa kupokea fedha za matokeo ambayo yaliyokuwa yamefutwa.

Wanaiomba serikali kupitia baraza la Mitihani kupitia upya uamzi wake wa kuwafutia matokeo watoto 111 wa sekondari ya Manchira ,pia Tume iliyoundwa na Waziri Mkuu Mizengo Pinda ifanye uchunguzi ili kubaini ukweli kwa kutumia barua za baraza za kudai malipo ili watoe matokeo wakati wakijua hakuna matokeo yatakayotolewa.

Ofisa elimu Sekondari wilaya ya Serengeti William Makunja amekiri kupokea nakala ya barua hiyo iliyotumwa na wazazi kwenda Baraza la Mitihani na kudai kama wilaya nao wanafuatilia.
Juhudi za kumpata msemaji wa baraza la Mitihani zinaendelea ili kutoa ufafanuzi wa malalamiko hayo.

Mwisho. inaendelea

0 comments:

Post a Comment