Subscribe:

Ads 468x60px

AKATA MIGUU NG'OMBE 27


AKATA MIGUU NG’OMBE 27 BAADA YAJARIBIO LA KUMUUA MAMA YAKE KUSHINDWA,
“Mtuhumiwa aliiba kuku anayeatamia na kuuza kwa sh.7.000 akanunua gongo,alipoulizwa akampiga mama yake aliyejiokoa kwa kumkamata nyeti kijana wake”
Septemba 21,2013

MKAZI wa kijiji cha Bwitengi kata ya Manchira wilayani Serengeti Witiribani Thomas Barangwa (30)anatuhumiwa kukata  miguu ng’ombe 27 wenye thamani ya zaidi ya sh,mil.5kufuatia ugomvi baina yake na mama yake aliyemtuhumu kuiba na kuuza  kuku kwa ajili ya kupata pesa ya kununulia pombe.

Tukio hilo ambalo limezua mjadala  kutoka kwa wananchi linadaiwa kutokea septemba 19 majira ya saa 7:00 usiku mwaka huu katika kitongoji cha Mewara limethibitishwa na Mwenyekiti na ofisa mtendaji wa  serikali ya kijiji Daud Manteni na Antony Makuru,na kuwa mtuhumiwa ametoroka anatafutwa.

Akielezea mkasa huo ofisa mtendaji alisema mtuhumiwa huyo aliamua kukata miguu ng’ombe hao baada ya kumsaka mama yake mzazi NyambiseThomas Barangwa na dada yake Loyce Thomas Barangwa waliompiga kutokana na kosa la kuiba kuku aliyekuwa ameatamia na kumuuza  kwa sh.7.000 na kwenda kunywa pombe za kienyeji.

“Katika ugomvi huo mtuhumiwa huyo alifanikiwa kumwangusha mama yake na kuanza kumkaba shingo…dada yake akaingilia kati, hata hivyo mama yake alipoona amezidiwa akamkaba sehemu za siri kwa nguvu na kumwachia…mtuhumiwa akakimbilia ndani na kuchukua silaha na kuanza kuwasaka awakate”alisema.

Makuru alisema mtuhumiwa alichukua panga kwa lengo la kumuua mama na dada yake ambao walikimbia na kujificha,na wanakijiji wakijitokeza kwa wingi kutoa msaada.

“Baada ya kuwakosa na kuona wananchi wamejitokeza kuwasaidia hasira zake zilihamia zizini na kuanza kukata ng’ombe mmoja baada ya mwingine mali ya baba yake…waliowekeshwa na wa kwake watatu hakuwagusa”alisema.

Baadhi ya mashuhuda walisema kuwa mtuhumiwa aliuza kuku anayeatamia na kuwa mchezo huo ulikuwa wa mara kwa mara na fedha zote akazitumia kwa kununua gongo,na alipoulizwa alikuwa mkali na kuwatishia.

“Akishakunywa pombe ni mkali sana si kwa mama yake wala majilani…na anatumia nafasi hiyo kwa kuwa wanaishi na mama yake tu…kwa kweli tukio alilofanya ni la kipekee na halijawahi kutokea kijijini hapa”alibainisha jilani ambaye hakutaka jina lake liandikwe.

Kutokana na tukio hilo wafanya biashara wa bucha wanadaiwa kununua ng’ombe hao kwa bei ya chini kwa kuwa hawakuwa na uwezekano wa kupona kutokana na jinsi walivyokuwa wamejeruhiwa,pia wakazi wa kijiji hicho walinufaika kwa kupata nyama.

Polisi wilayani hapa wanaendelea na msako dhidi ya mtuhumiwa na wanaomba wananchi watoe ushirikiano ili aweze kukamatwa na kufikishwa katika vyombo vya dola.
Mwisho.