Subscribe:

Ads 468x60px

JELA MIAKA MINANE KWA KUKUTWA NA MENO YA TEMBO


ALIYEKUTWA NA MENO YA TEMBO AHUKUMIWA MIAKA 8 JELA.
Serengeti:MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi mfawidhi wa wilaya ya Serengeti imemhukumu  Idd Abdallah Adamu (39 ) mkazi wa Nyakato Mwanza miaka 8 jela kwa kosa la kupatikana na  meno ya tembo  kilo 46 yenye thamani ya sh, 26,250,000 .
Katika kesi hiyo ya uhujumu uchumi namba 59/2011 washitakiwa wengine kwenye shitaka hilo   Lameck James (29) mkazi wa Sirari, Kasika John(46) mkazi wa Ushashi Bunda na Mwita John(44) mkazi wa kijiji cha Kibeyo wilaya ya  Serengeti  wameachiwa huru kutokana na udhaifu wa polisi kushindwa kuwasilisha fedha sh.3,835,000 walizokutwa nazo  mahakamani kama ushahidi  siku ya tukio.
Hakimu Amon Kahimba wa mahakama hiyo alisema,mshitakiwa Adamu amekumbwa na adhabu kufuatia ushahidi uliowasilishwa mahakamani hapo kuanzia maelezo ya polisi ,mahakamani na mashahidi kuwa vipande vinne vya meno ya tembo vilikutwa ndani ya chumba alichokuwa amelala nyumba ya wageni ya Leopard.
Na kuwa alikiri kununua meno hayo,kwa washitakiwa  wawili kwa sh,2,400,000 na washitakiwa Lameck James na Kasika John walikiri kununua vipande  hivyo vya meno kwa mshitakiwa wanne Mwita John kwa sh,200,000,na fedha walizokutwa nazo hotelini sh,3,835,000 hazikuwasilishwa mahakamani kama kielelezo licha ya washitakiwa kuzidai.
“Kutokana na maelezo yote ya ushahidi na washitakiwa ,mahakama inamhukumu Idd Abdallah miaka minane jela…na wengine wanaachiwa huru kutokana na uzembe wa polisi..wote hawa wangehukumiwa kama mpelelezi wa kesi na aliyekuwa Oc Cid wilayani hapo kwa sasa Mkuu wa Operesheni Mkoani Arusha Paul Ngonyani aliyewakamata,kuwapekua,lakini hakufika kutoa ushahidi mahakamani licha ya kuitwa na wala fedha alizowakutana nazo hazikuwasilishwa kama ushahidi”alisema.
Alikwenda mbali hakimu huyo na kudai kuwa kosa la kujihusisha na biashara ya meno ya tembo mazingira yake  wangekutwa na mzigo au pesa,lakini wao walikutwa na pesa katika nyumba ya kulala wageni ya Galaxy Motel ,lakini hazikuwasilishwa mahakamani.
Aliomba jeshi la polisi nchini liwachukulia hatua kali Paulo Ngonyani ,kwa kushindwa kufika kutoa ushahidi kwenye kesi hiyo licha ya kuitwa mara tatu,na mpelelezi wa shitaka hilo Ditektivu Sajenti Yona,kwa  kutowasilisha fedha za washitakiwa ambazo wamezidai na mahakama ikaagiza ziwasilishwe mahakamani..
Mapema mwendesha mashitaka inspekta msaidizi wa Polisi Abdallah Idd aliitaka mahakama hiyo kutoa adhabu kali kwa mshitakiwa ili liwe fundisho kwa wengine kwa kuwa makosa ya uhujumu uchumi yamekithiri hapa nchini.
Katika utetezi wake Adamu aliomba ahurumiwe kwa kuwa ni kosa lake la kwanza ,ana watoto 5,mke na watu wanaomtegemea.
Februari 18,2013 katika mahakama hiyo mshitakiwa huyo aliyehukumiwa aliyekuwa akijifanya Mmachinga anayetembeza vyombo kutoka Mwanza  aliachiwa huru na mahakama hiyo katika kesi 184/2011 ya uhujumu uchumi baada ya kukamatwa katika nyumba ya kulala wageni ya Silent Inn mjini Mugumu wakiwa na meno mawili ya tembo.
Katika kesi hiyo ilimhusisha mmiliki wa nyumba hiyo Julius Mwita Marwa(43)waliachiwa na Hakimu Amon Kahimba kwa kutumia kifungu cha sheria namba 235 cha mwenendo wa makosa ya jinai kilichorekebishwa mwaka 2002 kwa madai kuwa upande wa mashitaka ulikuwa dhaifu.
Mwisho.