Subscribe:

Ads 468x60px

MKATABA WA ULINZI WA MALIASILI WASAINIWA


 
 TANZANIAYATILIANASAINI NA THAILAND MKATABA WA KULINDA  MALIASILI NA KUKOMESHA UJANGILI,
Julai 31,2013.
Serengeti:SERIKALI ya Tanzania imetiliana saini mkataba wa maelewano  wa miaka mitatu wa ushirikiano wa kulinda na kuendeleza maliasili na Utalii na Jamhuri ya Kifalme ya watu wa Thailand.

Mkataba huo umesainiwa na Waziri wa Maliasili na Utalii balozi Khamisi Kagasheki kwa niaba ya serikali ya Tanzania  na Naibu Waziri Mkuu wa Thailand Plodprasop Suraswad  aliyeambatana na Waziri Mkuu wa Thailand Yingluck Shinawatra kwenye ukumbi wa  Four Session Safari Hotel Ltd  iliyoko hifadhi ya Taifa ya Serengeti.

Akizungumzia manufaa ya mkataba huo Waziri Kagasheki amesema hatua hiyo itasaidia taifa kuongeza mapato kupitia sekta ya Maliasili kwa kuongeza watalii kutoka milioni moja kwa sasa kama ilivyo kwa nchi ya Thailand pamoja na raslimali chache wanapata watalii hadi milioni 22 kwa mwaka.

“Tunataka mchango wa maliasili  katika pato la Taifa utoke asilimia 17  …hali hiyo ikienda sambamba na kuongeza pato la wananchi….maana Thailand kupitia utalii pato la Mwananchi ni dola 5,000 kwa mwaka …na ndio mpango  wa taifa wa 20-25”alisema.

Waziri wa uwezeshaji na Uwekezaji  Dk,Mary Nagu amesema mkataba huo unafungua fursa za uwekezaji ambao utainua pato la taifa katika sekta ya utalii,pia kilimo na madini.

“Tanzania tuna fursa nyingi lakini hatujafanya vizuri kwa ajili ya kujipatia mapato….tuna maliasili nzuri na kubwa tunawazidi Kenya …lakini wao wana vitanda 11,000 wakati sisi tunavitanda 6,000 sasa tunakusudia kukuza kwa kasi sekta hii kwa kushirikiana na nchi ambazo zinamwelekeo na zinazofanya vizuri”alisema.

Alisema ili kuhakikisha watanzania wananufaika na uwekezaji kama huo ,kwa upande wa madini serikali haitauza madini ghafi bali kuyatengeneza na kuwa vito ili yaongezewe thamani ,na watanzania wakipewa fursa ya kwanza kwa kuangalia watakavyonufaika.

Alisema ziara hiyo imekuja siku chache baada ya viongozi wa mataifa ya China,Marekani na Uingereza kutiliana mikataba ya kimaendeleo na taifa la Tanzania..

Mkurugenzi wa Wanyamapori Tanzania  Profesa Alexander Songorwa alisema ,wanategemea kuimarisha utalii na kupunguza tatizo la ujangili kwa kuwa nchi hizo zote zitahusika katika masuala ya ulinzi na usimamizi.

“Soko la meno ya Tembo kutoka Tanzania ni kubwa nchini Thailand na China …kwa mkataba huu sasa nao watashiriki kukabiliana na vitendo hivyo vya uharifu,na hiyo nafasi itatusaidia sisi kudhibiti hali hiyo…maana ujangili wa tembo ni changamoto kubwa kwa uhifadhi hapa Tanzania”alisema.

Mapema Mhifadhi Mkuu wa hifadhi ya Taifa ya Serengeti William Mwakilema akitoa taarifa ya hifadhi hiyo alisema mbali na kuwa kivutio kikubwa kwa wageni,bali wanakabiliwa nanchangamoto za askari wachache wa ulinzi wa wanyama pori,nyumba za askari ,maji ,barabara za ndani na jamii zinazowazunguka .

Kwa upande wa falme za Thailand walisema ,Raslimali za Tanzania zikilindwa na kusimamiwa vema zitasaidia kuinua uchumi kwa kasi kubwa,kwa kuwa wana vitu ambavyo havipo katika maeneo mengine,lakini hawajafanya vizuri.

Mwisho.

NAIBU WAZIRI MKUU WA THAILAND PLODPRASOP SURASWAD AKITIA SAINI YA MAKUBALIANO YA ULINZI WA MALIASILI NA WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII HAMISI KAGASHEKI UKUMBI WA HOTELI YA FOUR SESSION SAFARI LTD ILIOKO HIFADHI YA TAIFA YA SERENGETI
 SAINI YA MAKUBALIANO
 WAZIRI MKUU WA THAILAND YINGLUCK SHANAWATRA AKIANGALIA MCHORO WA MZUNGUKO WA NYUMBU
WANAKABIDHIANA MKATABA WA MAELEWANO