Subscribe:

Ads 468x60px

JK aunda Tume kuchunguza Operesheni Tokomeza Ujangili



Rais Jakaya Kikwete 
Na Mwandishi Wetu Mwananchi

Posted  Mei3  2014  saa 9:40 AM
Dar es Salaam. Rais Jakaya Kikwete ameunda Tume ya Uchunguzi, kuhusu vitendo vilivyotokana na Uendeshaji wa Operesheni Tokomeza.
Taarifa ya Katibu Mkuu Kiongozi Balozi Ombeni Sefue ilisema, Rais ameunda Tume hiyo kwa mujibu wa kifungu cha tatu cha Sheria ya Uchunguzi Sura ya 32.
Kutokana na hatua yake ya kuunda Tume hiyo, Rais Kikwete amemteua Jaji na Balozi Mstaafu Hamisi Msumi kuwa Mwenyekiti wa Tume hiyo.
Vilevile, Rais Kikwete amewateua Jaji Mstaafu Stephen Ihema na Jaji Mstaafu Vincent Lyimo kuwa Makamishna. Rais pia amemteua Frederick Manyanda, Wakili wa Serikali katika Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kuwa Katibu wa Tume hiyo.
Hatua ya Rais Kikwete kuunda tume hiyo inakuja baada ya Operesheni Tokomeza Ujangili kusitishwa na Bunge kutokana ukiukwaji wa sheria na haki za binadamu wakati wa utekelezaji wake.
Operesheni hiyo iliayoanza Oktoba 2013 na kusitishwa Nobemba 4 mwaka jana, ndiyo iliyowang’oa mawaziri wanne kwa kushindwa kusimamia vizuri utekelezaji wake.
Mawaziri hao ni Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Shamsi Vuai Nahodha, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk. Emmanuel Nchimbi, Waziri wa Maliasili na Utalii, Balozi Khamis Kagasheki na Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi, Dk Mathayo David Mathayo.
Taarifa ya Balozi Sefue inasema kuwa uteuzi huu ulianza jana, na kutaja majukumu ya tume hiyo kuwa ni pamoja na kuchunguza na kubaini Operesheni Tokomeza ilivyoendeshwa.
Majukumu mengine ni kuchunguza na kubaini iwapo Sheria, Kanuni, Taratibu na Hadidu za Rejea zilifuatwa na watu waliotekeleza Operesheni Tokomeza na kuchunguza na kubaini iwapo yupo mtu yeyote aliyekiuka Sheria, Taratibu na Hadidu za Rejea wakati wa Operesheni Tokomeza.
Kuchunguza na kubaini kama wapo watu wowote waliokiuka Sheria yoyote wakati wa utekelezaji wa Operesheni Tokomeza na kupima kama hatua zilizochukuliwa dhidi yao au mali zao zilikuwa stahiki.
Kupendekeza hatua zozote zinazopaswa kuchukuliwa dhidi ya mtu yeyote atakayebainika kukiuka Sheria, Taratibu na Hadidu za Rejea za Operesheni Tokomeza.
Kupendekeza mambo ya kuzingatiwa wakati wa kuandaa na kutekeleza operesheni nyingine siku zijazo ili kuepuka kasoro.





0 comments:

Post a Comment