Subscribe:

Ads 468x60px

Werema alikoroga, alinywa: Atoa kauli ya kuwabagua Wazanzibari



Posted  Ijumaa,Mei16  2014  saa 7:57 AM
Kwa ufupi

“Alichokizungumza Mnyaa ni sahihi lakini hapa si mahali pake, namshauri kuwa akaulize huko Zanzibar kwenye vikao vyao hapa sisi hatuna majibu,” alisema Werema.
Dodoma. Kwa maneno ya siku hizi ni kwamba Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Jaji Fredrick Werema ‘amelikoroga na kulinywa mwenyewe’, baada ya jana kutoa kauli ya kuudhi alipomtaka mbunge kutoka Zanzibar akaulize swali lake visiwani humo, iliyosababisha baadhi ya wabunge kususia Bunge na kutoka.
Kauli iliyoonyesha kuwagawa wabunge katika mafungu mawili; wa bara na Zanzibar, ilimlazimu Jaji Werema baadaye kusimama bungeni na kuwaangukia akiwaomba radhi waliokerwa na kauli yake na pia kuliomba radhi Bunge, Spika wake, Anne Makinda na wananchi.
Kuondoka kwa wabunge hao kulitokana na mwongozo wa Spika ulioombwa na Mbunge wa Ole (CUF), Rajabu Mbarouk Mohamed kutokana na majibu Jaji Werema kwa mbunge wa Mkanyageni (CUF), Habibu Mnyaa aliyekuwa ameomba ufafanuzi wakati Bunge lilipokaa kama kamati ya kupitisha vifungu vya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Katiba na Sheria kwa mwaka 2014/15.
Mnyaa alisema Wizara ya Katiba na Sheria ni muhimu lakini imekuwa ndiyo ya kwanza kuvunja sheria na haki za binadamu na akataka ufafanuzi.
Hata hivyo, aliposimama kujibu swali hilo, Jaji Werema alimwambia Mnyaa kuwa mambo mengine akaulize Zanzibar na siyo katika Bunge la Jamhuri kwa kuwa si kila kitu kitaulizwa ndani ya Bunge hilo.
“Alichokizungumza Mnyaa ni sahihi lakini hapa si mahali pake, namshauri kuwa akaulize huko Zanzibar kwenye vikao vyao hapa sisi hatuna majibu,” alisema Werema.
Mara baada ya Bunge kurejea, Mbarouk aliomba mwongozo wa Spika akitaka ufafanuzi wa kauli hiyo kwamba ilikuwa ya kibaguzi.
“Mheshimiwa Spika, huu ni ubaguzi na haupaswi kufanywa na mtu msomi kama Mwanasheria Mkuu wa Serikali,” alisema Mbarouk.
Alisema ubaguzi huo umewabagua wabunge ambao wamekula kiapo cha kulitumikia Bunge la Jamhuri ya Muungano na unaonyesha namna ambavyo Wazanzibari wanabaguliwa.
“Mheshimiwa Spika, yanapofanyika mambo kama hayo na wewe mwenyewe uko hapa unaona ni sawa na kubariki jambo hilo, huu ni ubaguzi unaoufanya wewe kwa kuwa lilifanyika ukiona bila hata ya kukemea,” alisema Mbarouk.
Hata hivyo, Spika alipinga na kusema: “Hakuna mwongozo wowote kwa kuwa hata wewe umevunja sheria kwani hata nilipokuambia kaa chini umeendelea kuzungumza, tunaendelea.... Katibu (akimtaka Katibu wa Bunge kutoa mwelekeo wa shughuli iliyokuwa inafuata ambayo ilikuwa Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi).”
Baada ya kauli ya Spika, wabunge wa Zanzibar walihamasishana na kuamua kutoka nje kwa wakati mmoja na huku wenzao wa upinzani wakiendelea kutafakari cha kufanya. Wakati huo, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mathias Chikawe alikuwa akisoma hotuba yake.
Muda mfupi baadaye, wabunge wa Chadema na NCCR Mageuzi nao walitoka na katika viti vya upinzani, alibaki John Cheyo wa UDP peke yake.
Baada ya kutoka
Akizungumza nje ya Viwanja vya Bunge, Mbarouk alisema wametoka kwa sababu Spika na Jaji Werema wamewadharau. “Hatutarejea ndani ya Bunge hadi hapo watakapotuomba radhi, wasipotuomba radhi hatutarejea bungeni,” alisema Mbarouk.
Hata hivyo, wakiwa nje ya Ukumbi wa Bunge, mbunge wa Wawi (CUF), Hamad Rashid Mohamed aliwafuata na kuwaeleza kuwa amezungumza na Werema na amekubali kuomba radhi kwa wabunge na Watanzania.
“Ndugu zangu nimeongea na Mwanasheria Mkuu wa Serikali, amekubali kuomba radhi,” alisema Hamad Rashid jambo ambalo liliungwa mkono na wabunge wa CUF waliokuwa wamekaa katika makundi katika Viwanja vya Bunge.
Hata hivyo, wabunge hao baada ya muda wa dakika 15, walikwenda katika kikao cha dharura kwenye Ukumbi wa Kambi ya Upinzani ambako pamoja na mambo mengine, walijadiliana kusudio la kumuona Spika Makinda kumweleza mambo yasiyowaridhisha.
Werema aomba radhi
Muda mfupi kabla ya Bunge kuahirishwa, Jaji Werema alisimama na kusema: “Kwa imani yangu, ninaamini kila binadamu ana nyongo, isipokuwa watu wawili... Yesu Kristo na Mtume Muhammad (SAW), ndiyo pekee ambao hawakuwa na nyongo. Naomba maneno yangu yafutwe katika kumbukumbu za Bunge hili.
“Mimi ni Jaji kwa taaluma na kwa nafasi yangu nimekosea kwa kutoa maneno hayo. Nimetambua kosa langu na naomba radhi... kwanza kwako Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rajab Mbarouk, Mheshimiwa Injinia Habib Mnyaa, Bunge hili na Watanzania kwa jumla.”
KULIKOROGA
“Alichokizungumza Mnyaa ni sahihi lakini hapa si mahali pake, namshauri kuwa akaulize huko Zanzibar kwenye vikao vyao hapa sisi hatuna majibu.”
KULINYWA
“Mimi ni Jaji kwa taaluma na kwa nafasi yangu nimekosea kwa kutoa maneno hayo. Nimetambua kosa langu na naomba radhi... kwanza kwako Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rajab Mbarouk, Mheshimiwa Injinia Habib Mnyaa, Bunge hili na Watanzania kwa jumla.”



Maswali 10 tata kuhusu dengue
http://www.mwananchi.co.tz/image/view/-/2316486/highRes/746639/-/maxw/600/-/1j259wz/-/mbu.png
“Lakini si lazima wawe wanazaliana zaidi katika maji masafi kwa sababu wana tabia ya kubadili tabia. Kwa mfano, anopheles wanaoeneza malaria nao walipenda maji masafi awali, lakini kwa sasa wamebadilika wanazaliana hata kwenye maji machafu,”.PICHA|MAKTABA 
Na Waandishi Wetu, Mwananchi

Posted  Ijumaa,Mei16  2014  saa 7:53 AM
Kwa ufupi
Dk Govela alisema suala hilo bado linahitaji utafiti zaidi kwa sababu kati ya aina tatu za mbu wanaosababisha dengue, hakuna utafiti uliofanyika kujua tabia zao wote.
Dar es Salaam.Tangu ugonjwa wa homa ya dengue uibuke mkoani Dar es Salaam na baadaye maeneo mengine ya nchi, wananchi wamekuwa wakijiuliza maswali mengi yenye utata ambayo sasa yamepata majibu ya wataalamu.
1. Kwa nini mbu wengine wakiwamo wanaoambukiza malaria hawawezi kuambukiza dengue?
Mtafiti wa tabia za mbu kutoka Taasisi ya Afya ya Ifakara (IHI), Dk Nicholaus Govela alisema mbu anayeambukiza homa ya dengue, Aedes Egypti, hawezi kubeba vimelea vya malaria wala yule anayeambukiza malaria hawezi kuambukiza dengue kutokana na maumbile yao.
Dk Govela alisema fiziolojia ya mwili wa mbu haiwezi kuruhusu Aedes Egypti kubeba virusi vya mbu mwingine.
“Ndiyo maana mbu hawezi kuambukiza Virusi vya Ukimwi,” alisema.
2. Kwa nini mbu wa dengue huuma mchana?
Dk Govela alisema suala hilo bado linahitaji utafiti zaidi kwa sababu kati ya aina tatu za mbu wanaosababisha dengue, hakuna utafiti uliofanyika kujua tabia zao wote.
Aina hizo ni Aedes Egypti, Aedes Albokictus na Aedes Africaans.
Alibainisha kuwa katika tafiti zinazofanyika, IHI iliwahi kubainika kuwa Aedes African ambaye pia anaambukiza dengue huuma usiku.
Alisema wengi wanamwelezea mbu huyu kwa kumlinganisha na tabia za mbu wa Japan, China na America ya Kusini lakini inawezekana huyu aliyepo hapa ni mpya tofauti na wa nchi za nje.
3. Je, dawa inayopulizwa inafaa kuwaangamiza?
Dk Govela alisema inawezekana ndiyo au hapana, lazima hili pia lifanyiwe utafiti kwa kuwa upo uwezekano wa mbu hawa kujenga usugu wa dawa kwa kuwa wamekuwapo nchini kwa miaka mingi.
Alipongeza uamuzi wa Serikali wa kupuliza dawa kwenye mabasi ya mikoani lakini bado alihoji iwapo imefikiria udhibiti kuanzia katika viwanja vya ndege na iwapo itawezekana kuzuia watu wanaokwenda mikoani wakiwa tayari wameambukizwa.
4. Je, kuna watu wanaougua dengue bila kuonyesha dalili?
Mtafiti huyo alisema wapo wanaougua bila kuonyesha dalili na wanaendelea kuambukiza... “Hawa mara nyingi hawaendi hospitali lakini wanakuwa na virusi mwilini,” alisema.
5. Kuna aina ngapi za virusi vya dengue?
Dk Govela alisema zipo aina nne za virusi vinavyoambukiza dengue. Alivitaja kuwa ni den 1, den2, den 3 na den 4. Hadi sasa, wanasayansi hawajaweza kubaini ni virusi vya aina gani vinasababisha homa hiyo kwa Tanzania.
“Ndiyo maana tunahitaji kufanya tafiti zaidi,” alisema.
6. Je, juisi ya majani ya papai ni tiba ya dengue?
Ofisa wa Taaluma na Udhibiti wa Magonjwa wa Shirika la Afya Duniani (WHO), Dk Grace Saguti alisema haijathibitishwa kisayansi.
Dk Saguti alisema ili tiba ikubalike, lazima ithibitishwe na hakuna namna mbadala ya kuiruhusu itumike kabla ya kujua madhara na faida zake. Alisema mpapai unaongeza vitamini A na hivyo kuimarisha kinga ya mwili, lakini si kutibu virusi vya dengue ambavyo kwa asili yake havina dawa.
7.Mbu wa dengue wako Dar es Salaam pekee?
Mtaalamu wa IHI alisema mbu huyo anaishi katika maeneo ya kitropiki, hivyo huenda yupo hata katika mikoa mingine. Alisema kwa tabia, aedes africans anafanana na mbu aina ya culex ambaye anapatikana katika mikoa mingine, hivyo hata huyo anaweza kuwapo huko pia... “Lazima ufanyike utafiti ili tujue iwapo mbu huyo hawezi kuzaliana katika mikoa mingine,” alisema.
8. Kwa nini aedes hupenda maji masafi yaliyotuama?
Dk Govela alisema ni kutokana na asili ya maumbile yao. Mbu hao huamini maji masafi yaliyotuama huwapa joto zaidi kwa ajili ya kutaga mayai.
“Lakini si lazima wawe wanazaliana zaidi katika maji masafi kwa sababu wana tabia ya kubadili tabia. Kwa mfano, anopheles wanaoeneza malaria nao walipenda maji masafi awali, lakini kwa sasa wamebadilika wanazaliana hata kwenye maji machafu,” alisema
9.Kwa nini wahudumu wa afya wanaathirika zaidi?
Daktari Kiongozi na Mtaalamu wa Homa ya dengue, Mrisho Lupinda alisema nao ni binadamu kama wengine na wanaishi maeneo hatarishi yenye mbu kama watu wengine.
10. Kwa nini panadol pekee ndiyo inatibu dalili za dengue?
Dk Lupinda alisema dawa nyingine za maumivu yaani Diclopar, Diclofenac na Aspirini huingiliana na mfumo wa chembe hai nyeupe za damu na huweza kusababisha chembe hizo kupungua mwilini. Dawa hizo huchochea kutengeneza sumu ambayo huathiri baadhi ya ogani za mwili.
Ugonjwa wasambaa
Homa ya dengue imesambaa katika maeneo mbalimbali nchini na kutoka Shinyanga, Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Mkoa, Fredrick Mlekwa amesema kumetokea kifo cha mtoto aliyekuwa na dalili zote za ugonjwa huo.
Huko Arusha, mkazi wa Maji ya Chai, Frank Nnko (30) amelazwa katika Hospitali ya Mkoa ya Mount Meru akitokea Hospitali ya Wilaya ya Meru akiwa na dalili za homa hiyo.
Zanzibar, wagonjwa watatu wanaodhaniwa kuwa na homa ya dengue wamelazwa katika Hospitali Kuu ya Mnazi Mmoja. Waziri wa Afya, Juma Duni Haji alisema wagonjwa hao wana dalili za ugonjwa huo.
Mtu mmoja amelazwa katika Hospitali ya Tumbi akiwa na dalili za dengue, akiwa na maumivu ya kichwa na kutoka damu puani, Ofisa Habari wa Hospitali hiyo, Gerald Chami alisema mgonjwa huyo mwenye umri wa miaka 30, alitokea Mbezi Wilaya ya Kinondoni.
Imeandikwa na Florence Majani, Andrew Msechu, Stella Ibengwe na Happy Lazaro, Mwinyi Sadallah, Talib Ussi na Julieth Ngarabali.


0 comments:

Post a Comment