Subscribe:

Ads 468x60px

Kila Mtanzania ana deni la Sh. 470,000





Ni mgawanyo wa deni la taifa la trilioni 21.2


Deni  la Taifa limeendelea kupaa na sasa limefikia Sh. trilioni 21.2 kiwango ambacho kama kikigawanywa kwa kila Mtanzania wanaofikia milioni 45 kwa sasa kwa usawa, kila mmoja atatakiwa kulipa Sh. 471,111.

Kiwango hicho cha deni kimepanda kutoka Sh. trilioni 16.98 cha mwaka wa fedha 2011/12.

 Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Ludovick Utouh, aliweka hadharani deni hilo jana wakati akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari mjini hapa juu ya ripoti ya ukaguzi kwa mwaka wa fedha 2012/13 ambayo inaishia Juni 30, mwaka jana. Ripoti hiyo iliwasilishwa bungeni.

Utouh alisema ongezeko hilo limesababishwa na mikopo kutoka kwenye mabenki na nchi wafadhili kwa ajili ya kusaidia miradi mikubwa ya maendeleo.

Utouh alisema deni la nje limefikia Sh. trilioni 15 hadi Juni 30, 2013  ambalo ni ongezeko la Sh. trilioni 3.0 kutoka Sh. trilioni 12.43 kwa mwaka 2011/12, wakati lile la ndani limefikia Sh. trilioni 5.78 ikiwa ni ongezeko la Sh. trilioni 1.23 kutoka Sh. trilioni 4.55 kwa mwaka 2011/12.

 “Ni maoni yangu kwamba, pamoja na deni la Taifa kuongezeka, uchumi wa nchi nao umekuwa ukiimarika kutokana na utekelezaji wa miradi mbalimbali,” alisema Utouh.

MISAMAHA YA KODI
Akizungumzia misamaha ya kodi, CAG alisema ukaguzi huo umebaini kuwa hadi kufikia Juni 30, mwaka jana Sh. trilioni 1.52 zilitolewa kama misamaha ya kodi.

 Alisema mwenendo umeonyesha kuwa kiasi hicho kimepungua kutoka Sh. trilioni 1.81 mwaka 2011/12 hadi Sh. trilioni 1.52 mwaka 2012/13 ambao ni upungufu wa Sh. bilioni 290.60 (asilimia 16).

 “Hivyo naipongeza serikali kwa hatua walizochukuwa kupunguza misamaha ya kodi kwa kiasi hicho ikilinganishwa na bajeti nzima ya serikali kwa mwaka 2012/13, misamaha ya kodi ambayo ilifikia asilimia 10 ya bajeti yote,” alisema.  Alishauri serikali izidi kupunguza kasi ya misamaha ya kodi ili fedha hizo zibakie serikalini na kufanya shughuli za maendeleo.

MWENYEKITI PAC
Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC), Zitto Kabwe, alipongeza ukaguzi huo kubaini mambo mbalimbali ikiwa ni pamoja na kunusuru fedha za walipakodi.

Alisema ripoti hiyo itaanza kufanyiwa kazi kuanzia sasa hadi Novemba ili kutoa maelekezo kwa hatua mbalimbali ambazo serikali itapashwa kuzichukua.Akizungumzia misamaha ya kodi, Zitto, alisema pamoja na kupunguza kiasi hicho hadi kufikia asilimia tatu ya pato la taifa, lakini bado ni kikubwa na kushauri ifikie asilimia moja ya pato la taifa.

Alisema wanakusudia kuwasilisha muswada wa mfumo mpya wa Kodi ya Ongezeko la Thamani (Vat) wenye lengo la kudhibiti misamaha ya kodi, ambao alisema unapigwa vita na baadhi ya wabunge na baadhi ya wafanyabiashara wakubwa wa madini.

 HATI CHAFU
Utouh alisema serikali imetoa hati za ukaguzi 961 kati ya hizo, 131 zimetiliwa shaka wakati nane zikiwa haziridhishi na mbaya zikiwa sita.

Alisema ukaguzi huo ulifanywa kwa halmashauri 140, wizara na idara na taasisi za serikali 117, mashirika na taasisi za umma 93, miradi ya wafadhili 611 na kubaini kasoro hizo.

Alisema pamoja na kuwapo kwa hati hizo chafu na zisizoridhisha, mwelekeo wa hati za ukaguzi kwa ujumla unaonyesha kuimarika kwa utendaji wa serikali katika kusimamia makusanyo ya mapato na matumizi ya rasilimali za umma ikilinganishwa na miaka iliyopita.

Alisema katika wizara na Idara za Serikali zilikuwa 117 na kuwa walibaini hati 85 zinaridhisha, hati 30 zenye mashaka, hati isiyoridhisha ilikuwa moja na hati mbaya moja.

Kwa upande wa halmashauri, alisema zilikaguliwa 140 na kubaini hati zinazoridhisha 112, zenye mashaka 27, isiyoridhisha bila kuwapo mbaya wakati. Kwenye mashirika ya umma taasisi zilizokaguliwa zilikuwa 93 hati zinazoridhisha zilikuwa 92, yenye shaka moja, hakukuwa na hati siyoridhisha wala mbaya.

 Katika miradi ya wafadhili iliyokaguliwa ni 611 na kupata hati zinazoridhisha 527, zenye shaka 73, zisizoridhisha sita na mbaya tano.

 Alisema hati zenye shaka kwa upande wa serikali kuu zimeongezeka kutoka tano mwaka 2011/12 hadi kufikia 30 mwaka 2012/13 kiliwango ambacho kimeongezeka mara tano.
 

0 comments:

Post a Comment