Subscribe:

Ads 468x60px

TMF wajitosa mapambano ya dawa za kulevya



Waandishi wa habari wakiwa kazini

Na Elias Msuya, Mwananchi

Posted  Jumapili,Juni1  2014  saa 24:0 AM
Kwa ufupi
Yaandaa programu maalumu ya kuwawezesha waandishi wa habari kuripoti habari za uchunguzi wa dawa za kulevya.
Dar es Salam. Mfuko wa Habari Tanzania (TMF) umeanzisha programu ya uandishi wa habari za uchunguzi kuhusu mapambano ya dawa za kulevya nchini.
Akizungumza juzi katika uzinduzi wa programu tano zinazofadhiliwa na TMF, mwakilishi wa kitengo cha habari cha Umoja wa Mataifa nchini, Stella Vuzo alisema programu hiyo imechaguliwa mahsusi kutokana na tatizo la dawa za kulevya kukithiri nchini.
“Tanzania ni kati ya nchi za Afrika zilizoathirika na matumizi na usafirishaji wa dawa za kulevya. Takwimu za Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii zinaonyesha kuwa jumla ya watumiaji 20,626 walipatiwa matibabu katika vituo vya afya kati ya mwaka 2008 hadi 2011,” alisema Vuzo na kuongeza:
“Takwimu za Jeshi la Polisi zinazonyesha kuwa, tangu mwaka 2010 hadi Mei 2013, jumla ya kilo 742 za heroini, kilo 348 za cocaine, kilo 77 za bangi na kilo 16,335 za mirungi zilikamatwa.”
Vuzo aliongeza kuwa hadi Julai 2013, Watanzania 247 walikamatwa wakisafirisha dawa hizo katika nchi za Mauritius, Umoja wa Falme za Kiarabu, China, Pakistan, Brazil na Afrika Kusini. “Kwa takwimu za ndani, kati ya kesi 423 za matumizi na usafirishaji wa dawa za kulevya ni kesi moja tu iliyoamuliwa kati ya mwaka 2005 hadi 2013. Kuna ongezeko la vijana wanaosafirisha dawa hizo kwa matumaini ya kutajirika,” alisema Vuzo.
Hata hivyo, Kamishna wa Kitengo cha kupambana na dawa za kulevya cha Jeshi la Polisi, Godfrey Nzowa aliyehudhuria hafla hiyo, alisema tatizo hilo sasa linapungua kutokana na mikakati thabiti ya jeshi.
“Kwa sasa Jeshi la Polisi tunajivuna kuwa tumeidhibiti biashara ya dawa za kulevya kwa kiasi kikubwa. Uthibitisho ni kupanda bei kwa dawa hizo. Kwa sasa kilo ya cocaine inafikia hadi Sh50 milioni na heroini hadi Sh45 milioni. Hazipatikani kirahisi kwa sababu tumedhibiti,”
alisema Nzowa na kuongeza:
“Ni kweli biashara hii inafanywa na baadhi ya vigogo wa Serikali na wafanyabiashara wakubwa. Lakini wana mbinu kali sana, wako tayari kwa lolote.”
Waziri wa Kazi na Ajira, Gaudensia Kabaka aliyekuwa mgeni rasmi wa hafla hiyo, aliwataka waandishi wa habari kutumia kila mbinu ya taaluma yao kuibua mambo yatakayoisadia Serikali kupambana na uhalifu.
Awali, akimkaribisha Waziri Kabaka, Mkurugenzi wa TMF, Ernest Sungura alisema lengo la mfuko huo ni kuisaidia Serikali kuleta maisha bora kwa Watanzania.
“Tofauti na taasisi nyingine, TMF tunafadhili waandishi wa habari kuandika habari za vijijini zaidi kuliko mijini tu. tunataka sauti zao nao zisikike,” alisema Sungura.
Mbali na program ya dawa kulevya, TMF pia inafadhili program za utafutaji na uchimbaji wa mafuta, gesi na madini, Ukatili wa jinsia, Watangazaji wanawake na Wapiga picha za televisheni.

0 comments:

Post a Comment