Subscribe:

Ads 468x60px

MAJAMBAZI YA MIFUGO YAJERUHI WAWILI KWA RISASI.

Serengeti:
WATU wawili wamelazwa katika hospitali ya wilaya ya Serengeti baada ya kupigwa risasi na watu wanaodaiwa kuwa wezi wa mifugo wakati wanafuatilia nyayo.

Mganga mwandamizi katika hospitali hiyo Dk.Tanu Waryoba amewataja majeruhi hao kuwa ni Chacha Megera(39)na Marwa Nyakimwi(21) wote wakazi wa kijiji cha Nyahende wilayani hapa.

Amesema Megera alipigwa risasi mguu wa kushoto na Nyakimwi kwenye nyonga mguu wa kulia na kutokea paja la mguu wa kushoto,na kuwa wanaendelea vizuri baada ya kupata matibabu .

Megera akiwa kitanda namba 12 wodi ya wanaume alikolazwa alisema oktoba 28 majira kati ya saa 4-5 usiku mwaka huu kulitokea wizi wa ng’ombe 9 nyumbani kwao wakati wamelala.

“Mke wa kaka yangu Kibibi Ntare alipotoka nje kujisaidia alibaini wizi huo…alipiga yowe kwa kushirikiana na wanakijiji tukaanza kufuatilia nyayo tukiwa tunakimbia…kufika eneo la mto Nyahende …tukishangaa ghafla nikapigwa risasi mguu wa kushoto”alisema.

Alisema alishindwa kuendelea na safari hiyo kutokana na maumivu makali na kulazimika kurudishwa nyumbani na kupelekwa hospitali kwa matibabu.

“Mimi nilipigwa risasi kwenye saa 6 usiku nikiwa miongoni mwa vijana wenzangu tuliokuwa mstari wa mbele…tukiwa tunakwenda kwa kasi baada ya kuwepo ishara kuwa wezi hawako mbali…ghafla nilipigwa risasi upande wa kulia wa nyonga na kutokea kushoto…niliishiwa nguvu na kulala chini”alisema Marwa Nyakimwi.

Nyakimwi aliyelazwa kitanda namba 8 alisema ilibidi akimbizwe hospitali,huku wenzake wakisonga mbele na kufanikiwa kurudisha ng’ombe wote 9 na kukamata watuhumiwa watatu kati ya sita waliohusika na tukio hilo.

Hata hivyo polisi walifanikiwa kuwaokoa watuhumiwa watatu waliokamatwa na mmoja aliyetajwa kwa jina la Mwita Malitwa(40)amelazwa hospitali ya wilaya chini ya ulinzi wa polisi.

Polisi wanasema wanaendelea na mahojiano na baadhi ya watuhumiwa na inasemekana watuhumiwa waliofanikiwa kutoroka walikimbilia maeneo ya Gibaso wilayani Tarime.

Kuhusu bunduki iliyohusika walisema ni ya kivita kwa kuwa risasi zake zilibainika ni za SMG ambazo zinatumiwa na bunduki aina ya SRA pia.
Mwisho.
Chacha Megera mmoja wa majeruhi akiwa hospitali ya wilaya ya Serengeti akiuguza majeraha ya risasi aliyopigwa wakati wakifuatilia wezi wa ng'ombe