Subscribe:

Ads 468x60px

TEMBO AVAMIA KIJIJI NA KUUAA NG'OMBE MMOJA


TEMBO WAVAMIA KIJIJI NA KUUA NG’OMBE

Oktoba 7,2013

HOFU imetanda kwa wakazi wa kijiji cha Makundusi kata ya Natta wilayani Serengeti kufuatia kundi kubwa la tembo kuvamia kijijini na kusababisha kifo cha ng’ombe na uharibifu wa mazao.

Tukio hilo limethibitishwa na uongozi wa kijiji na ofisi ya wanyama pori wilaya kuwa limetokea oktoba 3 majira ya saa 8 arasili mwaka huu katika eneo la Makundusi ambapo inadaiwa tembo hao wamepiga kambi kwa zaidi ya siku mbili.

Mwenyekiti wa serikali ya kijiji hicho Juma Porini alisema kuwa siku ya tukio tembo  kati 30-40 waliokuwa wamepiga kambi jilani na kijiji hicho walivamia kundi la ng’ombe na kuchanga nyika wakati wanachunga.

“Wachungaji wakakimbia ..ng’ombe nao wakaanza kukimbia,lakini kuna tembo mmoja ambaye amekatika mkia ambaye inadaiwa mwaka jana na mwaka huu ameua ng’ombe alianza kufukuza ng’ombe na kufanikiwa kumnasa mmoja kwa mkonga”alisema.

Alisema kuwa baada ya kumnasa alimbamiza kwenye mti kisha akaanza kumkanyaga na 
kumtoboa toboa hadi akafa,kisha akaanza kutafuta wengine lakini wakawa wamekimbia.


“Mara baada ya mauaji hayo wakaondoka na kukaa jilani na mpaka wa kijiji..jioni wanarudi kijijini na kuharibu mazao,kwa ujumla wananchi walikuwa wamejitahidi kulima mahindi lakini kwa hali ilivyo hawataambua kitu,maana wanyama hawa wameamua kupiga kambi kabisa”alisema.

Alisema walilazimika kutoa taarifa ofisi ya wanyama pori wilaya ambao walisema hawana gari,na kuomba msaada kwa hifadhi ya Jamii(WMA)ambao nao hawakufika,hata kampuni ya Singita Grumeti Reserves hawakufika kwa wakati.

Na kuwa hata walipofika walidai hawana risasi hali inayotia shaka utendaji wake,kwa kuwa halmashauri ilipewa gari na kampuni ya Singita Grumeti Reserves kwa ajili ya kukabiliana na tatizo la tembo,pia kila mwaka wanalipwa sh.mil.200 na kampuni hiyo,ambazo hazijasaidia idara zaidi ya madiwani kulipana posho za vikao.

Mjumbe wa serikali ya kijiji hicho Peter Magari alisema wananchi wana hofu kubwa ya kupoteza maisha kwa kuwa mbinu walizokuwa wanatumia kufukuza tembo sasa hazina maana kwa kuwa tembo wanaonekana wamezizoea.

“Tumekuwa tukitumia tochi kubwa kwa kukusanyana na mwanga unakuwa mkali huku tunapiga kelele,tembo wanakimbia …lakini kwa sasa badala ya kukimbia wanatufukuza hii inaonyesha wazi wameishazoea …kama hali ni hivyo inatishia usalama wetu”alisema.

Alisema tembo huyo mwaka 2012 aliua ng’ombe wawili mali ya Charles Machera na Mwanzoni mwa mwaka huu ameua ng’ombe mmoja na tukio hilo ni tatu anafanya madhara hayo.

Kaimu afisa wanyamapori wilaya Cathbert Boma alikiri kupata taarifa na kuwa hawakuwa na gari na kudai kuwa wameishaweka utaratibu kwa askari wa idara hiyo walioko Grumeti wanatakiwa kutaarifiwa.

“Tatizo la tembo kuvamia maeneo ya vijiji linazidi kuongezeka kwa kuwa wanapokuwa wanawindwa ndani hukimbilia nje…kwa hiyo tatizo hili linasumbua sana maeneo mbalimbali “alisema.

Hivi karibu Tembo alivunja uzio na kumuua Faru aitwaye Limpopo aliyekuwa amehifadhiwa katika eneo la Kijiji hicho na kampuni ya Singita Grumeti Reserves.
Mwisho.