Subscribe:

Ads 468x60px

KULALIA JAMVI KWA MFANYA ACHOME GODORO LA JILANI YAKE NA KUMUUNGUZA MTOTO


 
 MTOTO KELVIN MARWA WA MIAKA MIWILI AMELAZWA KTK HOSPITALI TEULE YA NYERERE WILAYA YA SERENGETI   AKIWA NA MAMA YAKE JACKLINE ANAYEMUUGUZA MAJERAHA YA KUCHOMWA MOTO NA JILANI YAO KUTOKANA NA WIVU WA KULALIA GODORO WAKATI YEYE ANALALIA JAMVI

Serengeti:
WIVU wa kukosa godoro  umempelekea mwanamke  mmoja wa mtaa wa uwanja wa mbuzi mjini Mugumu wilayani Serengeti kuchoma godoro la jilani yake  na kumuunguza vibaya mtoto wakati amelala.
Tukio hilo la aina yake limethibitishwa na polisi wilayani hapa  na kumtaja mtuhumiwa kuwa ni Esther Juma  linadaiwa kutokea  oktoba 30 majira ya saa 1:00 asubuhi ambapo mtoto huyo aliyetajwa kwa jina la Kelvin Marwa(2)ameungua sehemu mbalimbali za mwili na amelazwa hospitali ya wilaya kwa matibabu.
Akisimulia mkasa huo mama mzazi wa mtoto huyo akiwa hospitalini  Jackiline Godfrey(20)alisema wamekuwa na ugomvi na mtuhumiwa ambaye ni jilani yake baada ya kuwa amenunua godoro na yeye analalia jamvi,na  siku hiyo akaamua kuchoma godoro na kumuunguza mwanae.
“Nilitoka saa 12:00 alfajiri kuwahi kibaruani stendi kwenye mgahawa ninakofanya kazi…nikaacha mwanangu amelala…hurudi mapema kumwandalia chai ama uji…nikiwa kazini majira ya saa 1:00 asubuhi  nilifuatwa na mtoto wa jilani..akasema Kelvin ameungulia ndani---niliishiwa nguvughafla…kwenda nikakuta majilani wamebomoa mlango na mtoto ameungua vibaya”alisema huku akifuta machozi.
Alisema mbali na mtoto kuungua pia nguo na vitu vingine viliungua  vyote kutokana na unyama huo uliofanywa na jilani yake ambaye amekuwa akimwapia kumkomesha kwa yeye kununua godoro na kumwacha yeye akilalia jamvi.
Baadhi ya mashuhuda walisema walimwona mtuhumiwa akitoka ndani ya chumba kilichoungua akikimbia ,ghafla wakaona moshi na sauti ya  mtoto  ikisikika akilia kwa sauti kali ,katika kufuatilia wakabaini mtoto anaungua wakabomoa mlango na kumnusuru mtoto huyo.
“Kilichomsadia mtoto baada ya kuanza kuungua alijivuta hadi kwenye kona na kuacha godoro linaungua….kwa kweli ni unyama mkubwa sana aliokuwa anaufanya huyo mwanamke….kulalia jamvi kunampelekea kutaka kumuua huyo mtoto…kwa kweli kama polisi wasingewahi angeuawa”alisema shuhuda.
Balozi wa nyumba 10 eneo hilo Janet Samwel alisema baada ya kukamatwa kwa mtuhumiwa alianza kupigwa na kama si polisi kufika eneo hilo mapema huenda angeuawa kwa kuwa wananchi walikuwa na hasira kali dhidi ya ukatili huo.
Mratibu wa dawati la jinsia la polisi wilaya WP 5665 D/S Sijali Nyambuche alisema walilazimika kufika haraka eneo la tukio baada ya kupata taarifa za tukio ,wakabaini kuwa huenda kukatokea maafa kwa mtuhumiwa kutokana na mazingira ya tukio na hasira za wananchi.
“Kama tusingewahi ingekuwa mbaya zaidi…tulimnusuru mtuhumiwa na tunamshikilia ..taratibu zikikamilika atafikishwa mahakamani wakati wowote”alisema.
Muuguzi wa zamu wodi ya watoto Mwangwa Samson alisema mtoto huyo ameungua makalio,miguu na sehemu za siri kwa asilimia 30 na kuwa hawezi kukaa kutokana na majeraha aliyopata,na juhudi za madaktari na waganga zinaendelea kuhakikisha anapona.
Mwisho.


 BAADHI YA VITU VILIVYOBAKI KATIKA CHUMBA WALICHOKUWA WANAISHI