Subscribe:

Ads 468x60px

SHULE MBILI ZENYE WATOTO 1,005 ZINA WALIMU WATANO,



kati yao watoto 777 husoma wamekaa chini,kutokana na ukosefu wa madawati.
Machi 10,2014
Serengeti:WALIMU watano  wa shule za msingi Kitarungu  na Matanka kata ya Nyansurura wilayani Serengeti wanalazimika kufundisha  wanafunzi 1005 ,moja yenye watoto 557 ina walimu 2 na nyingine yenye watoto 448 ina walimu 3.
Mbali na upungufu wa walimu shule hizo zote mbili zina madawati 76 ambapo wanafunzi 777 kwa shule hizo mbili husoma wamekaa chini hali ambayo inabainisha changamoto kwa sekta ya Elimu ambayo ni miongoni mwa sekta 5 zilizokwisha zindua mikakati ya Matokeo Makubwa sasa(BRN).
Mratibu elimu kata hiyo Benard Misolo aliliambia Mwananchi kuwa kwa hali hiyo wastaraji miujiza kwa walimu wawili kufundisha wanafunzi 557 kuanzia darasa la kwanza hadi la saba ,wakati huo Mwalimu mkuu ana majukumu ya utawala.
“Tatizo hili ni la muda mrefu ,ofisi ina taarifa ….kupitia uongozi wa kata na elimu toka mwaka 2007 shule ilipoanzishwa bila mafanikio…tukipata walimu sita watasaidia kupunguza tatizo ,kwa shule ya Matanka walimu watatu hawakidhi… wanaopata shida hapa ni watoto”alisema.
Kuhusu madawati alisema shule ya Kitarungu wanafunzi wanaosoma wamekaa kwenye madawati ni 108,huku wanafunzi 449 wanasoma wakiwa wamekaa chini,na shule ya Matanka wanaokalia madawati ni 120,huku 328 wanasoma wakiwa wamekaa chini.
“Kuna upungufu mkubwa wa vyumba vya Madarasa ,maana darasa moja watoto wanakaa kuanzia 50 hadi 120…wengi wakiwa wamekaa chini…hakuna usikivu hapo..hayo yote ni madhila yanayowakuta walimu wawili,”alisema.
Diwani wa kata ya Nyansurura Jackson Mwita(Chadema) aliliambia Mwananchi kuwa kata yake inahali mbaya kwa upande wa elimu kwa shule za msingi,kwa kuwa shule zote saba hazina walimu wa kutosha.
“Tumeomba sana walimu lakini hatupewi…wanadai hakuna nyumba za walimu…lakini hakuna kata yenye nyumba za walimu za kutosha….mjini shule moja ina watoto 800 ina walimu 37,hakuna nyumba wamepanga….hapa watoto zaidi ya 500 walimu wawili….uwiano gani huo…harafu mwisho unalaumu watoto na wazazi….nadhani kuna mitizamo hasi ya kisiasa,”alisema kwa masikitiko.
Mwenyekiti wa kamati ya Elimu,afya na Maji halmashauri hiyo Daniel Kegocha amekiri kuwepo kwa upungufu huo na kuwa lilikwishatolewa agizo idara ya elimu kupitia vikao kuwa wapeleke walimu shule zenye upungufu.
“Walimu wapya watakaporipoti mwaka huu shule zenye upungufu zitapewa kipaumbele…si hizo hata Nyahende kata ya Kebancha bancha ina walimu watatu wanafunzi zaidi 500…maana shule za mjini wamerundikwa walimu wengi lazima uwiano uwepo,”alisisitiza.
Hata hivyo imebainika kuwa shule nyingi hazina nyumba za walimu,na hata vijijini wanakosa nyumba za kupanga hali ambayo inapelekea walimu kukimbia,ambapo mwaka 2013 walimu 80 walihama mkoa huo,wengi wakilalamikia mazingira magumu ya kazi.
Uongozi wa idara ya elimu wilaya wamekiri kuwepo kwa upungufu na kudai kuwa tatizo kubwa ni ukosefu wa nyumba ,hata nyumba za walimu kupanga baadhi ya maeneo ni changamoto na kuomba jamii kujitolea kujenga nyumba ,na kutengeneza madawati ili kuboresha elimu.
Mwisho.