Subscribe:

Ads 468x60px

Tawla kutumia wanasheria 400 kutatua migogoro ya ardhi vijijini




Na Hadija Jumanne, Mwananchi

Posted  Ijumaa,Februari28  2014  saa 14:31 PM
Kwa ufupi


 Juma Nyamhanga(36)mkazi wa kijiji cha Nyamitita wilayani Serengeti akiwa hospitali Teule ya Wilaya ya Serengeti,kufuatia kukatwa mkono kutokana na mgogoro wa ardhi-picha na Mayunga Blog

  • Lengo la chama hiki ni kutoa msaada kwa watoto, wanawake na watu mbalimbali.”

Kila kukicha kumekuwa na kesi za migogoro ya ardhi, mirathi na hata kesi za wazazi kuozesha watoto wao yaani mimba za utotoni na ndoa za utotoni na hii ni changamoto kubwa inayoikabili nchi kwa sasa.
Utafiti uliofanywa hivi karibuni na Chama cha waandishi wa habari wanawake (TAMWA) umeonyesha kuwa katika kipindi cha mwaka 2012/2013 jumla ya matukio 228 ya mimba  na matukio  42 ya  ndoa za utotoni  yaliripotiwa huko Pemba na wilaya ya kati Unguja.
Hata hivyo, mimba na ndoa za utotoni  zimetajwa kuwa ni miongoni mwa vikwazo vinavyowapata watoto wa kike  kwamba tatizo hilo bado ni kubwa kwa baadhi ya maeneo ya Tanzania Bara na Visiwani.
Wakati  Tanzania Visiwani  hali ya ukatili dhidi ya wanawake na watoto ikionekana zaidi katika Mkoa wa Kusini Pemba na Wilaya ya Kati Unguja, upande wa Tanzania bara  maeneo yenye ukatili dhidi ya wanawake pamoja na mimba za utotoni yanaonekana katika wilaya za  Kahama, Tarime, Sengerema, Newala, Mbulu, Bunda, Nkasi, Babati, Chunya, Dodoma, Bariadi, Busega na Singida vijijini.
Bokhe Odhiambo (31), mkazi wa Tarime mkoani Mara, anasema vitendo vya ukatilli dhidi ya wanawake ndani ya ndoa na mimba za utoto kwa watoto wa kike ni mambo ya kawaida  na jamii wala haina muda wa kuyakemea.
“Kupigwa au kufanyiwa vitendo vya ukatili dhidi ya wanawake ndani ya ndoa, migogoro ya ardhi na mimba za utotoni kwa watoto wa kike ni mambo ya kawaida tu kwenye jamii yetu licha ya wasaidizi wa kisheria kutoa elimu,” alisema Odhiambo.
Kutokana na changamoto hiyo, Chama cha Wanasheria Wanawake Tanzania (Tawla) kimejitosa kutoa msaada wa kisheria katika mikoa yenye changamoto lengo likiwa ni  kupunguza tatizo hilo.
Mwenyekiti wa  Chama cha Wanawake Wanasheria Tanzania (TAWLA), Aisha Bade anasema kutokana na ukubwa wa tatizo hilo chama chake kimeamua kusambaza  wasaidizi wa kisheria  400 nchi nzima  lengo likiwa ni kusaidia kutatua migogoro ya ardhi na mirathi.
Bade anasema Tawla imebaini kuwa mikoa ya  Pwani na Morogoro, Mtwara, Lindi, Arusha , Tanga, Shinyanga, Manyara na Mwaza  inaongoza kwa kuwa na migogoro ya  mirathi, vitendo vya ukatili na  kuozesha watoto katika  ndoa za utotoni.
Anasema kuwa mbali na mikoa hiyo pia mikoa ya  Tanga, Arusha, Dodoma inaongoza kwa kuwa na migogoro ya ardhi pamoja na mirathi na hivyo juhudi mbalimbali zinahitajika kukabiliana na tatizo hilo. “Tumesambaza wasaidizi wa kisheria 400 nchi nzima  lengo ni kutatua migogoro iliyopo hasa katika maeneo ya vijijini ambayo tumeona hayana msaada wa kisheria” anasema Bade.
“Mbali na  mikoa hiyo pia mikoa ya  Tanga, Arusha, Dodoma nayo ni miongoni mwa mikoa  inayoongoza kwa kuwa na changamoto kubwa ya  migogoro ya ardhi na miradhi na kwamba  juhudi za pamoja  zinahitajika kushirikia katika kutatua changamoto hiyo ili kupunguza madhara yanayoweza kutokea kutokana na tatizo hilo”anasema Beda.
Anasema TAWLA ilianza mafunzo ya wasaidizi wa sheria mwaka 2006 na kutokana mafunzo hayo zaidi ya wananchi 4,600 wamenufaika kwa kupata msaada wa kisheria  vijijini katika kipindi cha mwaka jana pekee.
“Lengo la TAWLA kuanzisha mradi wa mafunzo  ni kuwapatia haki wananchi ambao hawana  uwezo wa kuwa na mawakili katika kushughulikia migogoro ya ardhi na miradhi na kwamba chama chetu kiliamua kuanzisha mradi huu kutokana  na nchi kukabiliwa na uhaba wa wanasheria  na mawakili na hivyo kuwa vigumu kwa watu wa vijijini kupata msaada wa kisheria katika kutatua matatizo yao,”alisema Beda.
Pia Beda  anasema  kuwa  ripoti  inaonyesha   hadi  sasa   wasaidizi  wakisheria   wameweza  kuwafikia  watu   6,000  pamoja  na  kutoa  elimu  kuhusu   sheria  na  haki   za  binadamu.
Anasema mpaka sasa chama hicho kimeshapokea  zaidi ya kesi 700 za usuluhishi wa ndoa , migogoro ya ardhi, migogoro ya miradhi na madai mbalimbali yanayotokana na matunzo ya watoto na hivyo kuzipatia msaada wa kisheria.
 “Licha ya kusambaza wasaidizi wa kisheria vijijini  bado nchi inakabiliwa na changamoto ya uhaba wa wataalamu hao  kutokana na mahitaji kuwa makubwa kuliko idadi ya wataalamu wa masuala ya kisheria,”anasema.
Nasieku  Kisambu, ambaye ni Kaimu Mkurugenzi wa Tawla, anasema licha ya kupeleka wasaidizi hao wa kisheria vijijini bado kuna changamoto ya uhaba wa wasaidizi wa kisheria nchini kutokana na mahitaji yaliyopo.
Kisambu anataja  mikoa yenye  wasaidizi wa kisheria kuwa ni Dodoma yenye wasaidizi 98, Morogoro 12, Katavi 73, Dar es Salaam 22, Pwani 8, Arusha 154 na Tanga  wasaidizi 45 ambao watatoa huduma hiyo kwa jamii bila gharama yoyote.
Kisambu anasema maeneo  yatakayonufaika na huduma hiyo ni yale ya vijiji ambayo jamii imeshindwa kupata haki  zao stahiki kutokana na kukosa msada wa kisheria na uhaba wa fedha kwa ajili ya kutafuta mawakili katika kusimamia kesi zao.
“Lengo la kuwepo kwa chama hiki  ni kutoa msaada wa kisheria kwa watoto, wanawake  na watu wenye matatizo mbalimbali ambayo ni migogoro ya ardhi na  mirathi”anasema Kisambu.
Kisambu anasema kutokana na uelewa mdogo wa masuala ya elimu juu ya unyanyasaji na ukatili kumekuwa na matukio ya mara kwa mara wanayofanyiwa wanawake na watoto lakini kupitia  wasaidizi wa kisheria wataweza  kutatua migogoro iliyopo nchini.
“Mikoa kama Morogoro, Mtwara, Lindi, Arusha , Tanga, Shinyanga, Manyara na Mwaza  inaongoza kwa kuwa na migogoro ya  mirathi, vitendo vya Ukatili na  kuozesha watoto katika  ndoa za utotoni na hali hii ya kuoza watoto wadogo inatokana na wazazi kutokuwa na uwezo wa kuwaendeleza watoto wao kielimu nan a badala yake huona kuwa badala ya mtoto kupata mimba akiwa nyumbani baada ya kumaliza darasa la saba ni bora aolewe ili kuondoa aibu”anasema Kisambu na kuongeza .
“Mwamko mdogo kwa baadhi ya jamii juu ya umuhimu wa elimu kwa mtoto wa kike unaendelea kukwamisha maendeleo ya wanawake na kuupa kipaumbele mfumo dume ambao kwa miaka mingi unapigwa vita na mataifa yote ulimwenguni” alisema Kisambu.
Kwanini migogoro ya ardhi.
Kaimu  Msajili wa Mabaraza ya Ardhi na nyumba ya wilaya nchini, Jane Kapongo anasema ufinyu wa bajeti ya serikali  kwa wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya makazi ni moja kati ya changamoto inayochangia kuendelea kwa migogoro ya ardhi nchini.
Kapongo anasema katika  kipindi cha mwaka 2012 na 2013 watu  58393 waliopata hati baada ya kupimwa viwanja vyao  nchi nzima na kwamba  jukumu la wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi ni kusimamia  sera  na kuweka miongozo ya matumizi ya ardhi pamoja na  kutatua migogoro.
Anasema  hadi Desemba mwaka 2011  wizara hiyo ilikuwa  imepokea asilimia 27.8 ya fedha zilizoidhinishwa kwa mwaka wa fedha 2011/12 hivyo kushindwa utekelezajiwa majukunu yake kwa ufanisi.
“Halmashauri nyingi hazitengewi bajeti  na hali hii inasababisha migogoro kutokana na  kiasi kidogo kinachotolewa katika bajeti  hakikidhi ulipaji wa fidia kwa wananchi, kushindikana upimaji viwanja, uendelezaji miji hushindwa kufanyika kwa sababu ya uhaba wa fedha na hatimaye  kusababisha migogoro”Anasema  Kapongo.
Anasema   jukumu la kupima na kugawa viwanja  linafanywa na  mamlaka za serikali za mitaa ambazo ni Halmashauri za wilaya, Miji, Manispaa na Majiji hivyo wizara  imekuwa ikijikita katika kusimamia sera na kuweka miongozo ya matumizi ya ardhi  na utatuzi wa  migogoro inayoibuka kila  mara.
Kapongo anataja  baadhi ya migogoro mikubwa ya ardhi iliyopo nchini kuwa ni migogoro kati ya jamii za wakulima na wafugaji,  wanavijiji na wawekezaji, migogoro ya mipaka baina ya mamlaka mbalimali na wamiliki wawili katika kiwanja kimoja.
“Migogoro mingine ni Uvamizi wa mashamba na viwanja,  wananchi kutoridhika na fidia inayolipwa wakati wa utwaaji ardhi na hali hiyo inatokana na elimu duni kwa jamii kuhusiana na  sheria, kanunia na taratibu za utawala wa ardhi”anasema Kapongo.
Anafafanua zaidi kuwa ukosefu wa uadilifu  kwa baadhi ya watendaji katika sekta  ya ardhi, upungufu wa watendaji na  vitendea kazi pamoja na utunzaji hafifu ya kumbukumbu ni moja kati ya sababu  inayochangia migogoro ya ardhi nchini.
Jinsi ya utatuzi wa migogoro ya ardhi unavyofanyika:
Kaimu Mkurugenzi wa Tawla, Nasieku Kisambu anasema sheria  ya mahakama za ardhi ya mwaka 2002 imeweka utaratibu na muundo mpya wa utatuzi wa migogoro ya ardhi nchini.
Miongoni mwa utatuzi huo ni kuwa na baraza la ardhi la kijiji ambalo jukumu lake ni  kusuluhisha migogoro ya ardhi inayotokea hapo kijiji.
Vile vile katika utatuzi huo wa migogoro ya ardhi lazima kuwe na baraza la ardhi la kata na baraza la ardhi  na nyumba la wilaya ambalo limeundwa na waziri anayehusika na masuala ya ardhi.
“Mabaraza haya yanatakiwa kuwepo katika ngazi zote za wilaya ili kuhakikisha huduma stahiki kwa wananchi inatolewa na kwamba kazi ya baraza hili ni kusikiliza  rufaa kutoka baraza la kata, kusikiliza mashauri mbalimbali ya ardhi kwa mujibu wa sheria  za ardhi pamoja na kusimia utekelezaji wa maamuzi yake”anasema Kisambu.
Nini kifanyike?
Kapongo anasema serikali iongeze banjeti kwa wizara hiyo ili kuwepo na wataalamu watakao weza kuwafikia wananchi wa vijijini na kutatua migogoro pamoja na kuwepo kwa  uadilifu  kwa baadhi ya watendaji katika sekta  ya ardhi na kuongeza  watendaji na  vitendea kazi katika maeneo husika.
Vile vile kutolewe elimu itakayosaidia kupunguza changamoto hiyo kwani migogoro mingi ya ardhi inatokana na kutoridhika na fidia inayolipwa wakati wa utwaaji ardhi na hali hiyo inatokana na elimu duni kwa jamii kuhusiana na  sheria, kanunia na taratibu za utawala wa ardhi.
Vile vile kwa upande wa ukatili, Beda anasema  licha ya kuwepokwa sheria zinazobidhitihali hiyo bado kuna changamoto ya uhaba wa wasaidizi wa kisheria katika maeneo mbalimbali ya nchi.