Subscribe:

Ads 468x60px

Jiepusheni na upotoshaji, Samia awaasa waandishi



Na Mwandishi Wetu, Mwananchi

Posted  Jumatatu,Marchi17  2014  saa 10:28 AM
Kwa ufupi
Waandishi wa habari wametakiwa kutumia kalamu zao kuijenga Tanzania na kujiepusha na upotoshaji unaoweza kuivuruga nchi.
Dodoma. Waandishi wa habari wametakiwa kutumia kalamu zao kuijenga Tanzania na kujiepusha na upotoshaji unaoweza kuivuruga nchi.
Wito huo ulitolewa jana na Makamu Mwenyekiti wa Bunge la Katiba, Samia Suluhu Hassan wakati akizungumza na waandishi wa habari katika semina iliyoitishwa na Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu (THRDC).
Semina hiyo ya siku moja ililenga kuwakumbusha waandishi wa habari umuhimu wa kufuatilia na kuibua mambo muhimu yanayoendelea ndani ya Bunge la Katiba.
“Nawaomba mjikite katika kuandika habari ambazo zitalenga kuweka mustakabali mzuri wa nchi yetu kuliko kuweka makombora ambayo hayana msingi wowote,” alisema Samia.
Alisema kalamu za waandishi wa habari zinaweza kuibua mambo mazito ambayo yakienda kwa mwelekeo mzuri, yatakuwa yanajenga nchi lakini yakipotoshwa itakuwa hatari zaidi.
Aliwakumbusha waandishi kuwa Watanzania wengi hivi sasa macho na masikio yao yameelekezwa Dodoma ambako Bunge linaendelea na mjadala wa Katiba, hivyo kila kinachofanyika wanakifuatilia kwa umakini mkubwa.
Samia, ambaye pia ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano), alisema anakerwa na uandishi unaolenga zaidi mambo ya Muungano na kuacha mengine muhimu ndani ya rasimu.
Suala la waandishi kuripoti shughuli za Bunge la Katiba liliibua mjadala, hasa baada ya baadhi ya wajumbe kutaka waandishi wasihudhurie vikao vya kamti za bunge hilo, nia ambayo ilihitimishwa kwa wajumbe kupitisha kanuni inayozuia waandishi kuhudhuria vikao vya kamati.
Vyombo mbalimbali vya habari vimepinga kanuni hiyo vikieleza kuwa inafinya uhuru wa habari.