Subscribe:

Ads 468x60px

Wako: Msipuuze maoni ya Wananchi



 
Mwanasheria Mkuu mstaafu wa Serikali ya Kenya, Seneta Amos Wako akizungumza jana, wakati wa Semina ya Bunge Maalumu la Katiba. Picha na Salim Shao 
Na Habel Chidawali na Editha Majura, Mwananchi

Posted  Ijumaa,Marchi21  2014  saa 9:11 AM
Kwa ufupi
  • Awataka Wajumbe wa Bunge la Katiba watunge Katiba inayotokana na maoni na matakwa ya wananchi ili kuepusha migogoro.
Dodoma. Mwanasheria Mkuu (AG) mstaafu wa Kenya, Amos Wako amewataka wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba kutokupuuza maoni ya wananchi katika kutunga Katiba ya nchi vinginevyo watazua mgogoro.
Wako, ambaye kwa sasa ni Seneta wa Busia ya Mashariki nchini Kenya, alitoa ushauri huo jana katika semina kwa wajumbe wa Bunge la Katiba kuhusu uzoefu wa namna nchi hiyo ilivyopitia misukosuko ya kuipata Katiba mpya.
Wako ambaye kwa miaka 21 alikuwa katika wadhifa wa AG, alisema matukio mengi yaliyosababisha Kenya kutokupata Katiba yao kwa wakati, yalitokana na kutokuwashirikisha wananchi moja kwa moja katika mchakato.
Katika hotuba yake iliyodumu kwa saa 2: 11, mwanasheria huyo aliyewahi kuwa Mwenyekiti wa Tume ya Katiba ya Kenya alionya pia kuwa Katiba inayotengenezwa hapa nchini isiwe ya kunukuu kutoka katika mataifa mengine kwa sababu mahitaji yanatofautiana kwa kila nchi.
“Katiba isiwe ya mazungumzo kutoka kwa viongozi pale Dar es Salaam, kwani itakuwa ni mali ya watu wachache na ambayo lazima itapingwa, hata sisi tulianza hivyo lakini tulishindwa vibaya,” alionya Wako.
Aliimwagia sifa Rasimu ya Katiba iliyowasilishwa bungeni Jumanne iliyopita, kwamba kwa mtindo ilivyowasilishwa inaonekana kuwajali na kuwapa nafasi zaidi wananchi wa hali ya chini.
“Pamoja na hayo, lakini Katiba hii ikiingiliwa zaidi na kutekwa na wanasiasa au kikundi cha watu wachache kwa masilahi yao, inaweza kuharibika kama ilivyotokea kwetu Kenya ambako Kanu walikuwa wakipinga kila kitu wakatufanya tuingie katika mgogoro.”
Alisema kuwa mitazamo ya wanasiasa huwa ni tatizo na hatari katika kutafuta Katiba mpya na dawa pekee na ya maana ni kutoa nafasi kwa wananchi waamue wenyewe.
“Mfumo uliowekwa katika mchakato wa kuunda Katiba mpya nchini kwenu, kwamba Rasimu ya mwisho ya Katiba itoke bungeni na kupelekwa moja kwa moja kwa wananchi ni mzuri, ni muhimu maoni ya wananchi ya awali yazingatiwe,” alisisitiza.
Kwa mujibu wa mwanasheria huyo, Bunge Maalumu limeaminika kufanya kazi hiyo ili kuwasaidia wananchi kufikia malengo yao.
Uzoefu wa Kenya
Akizungumzia uzoefu wa Kenya katika kupata Katiba mpya alisema walianza kwa kukabiliana na changamoto kubwa ya ukabila ambayo kila jamii ilikuwa haiamini kundi jingine katika kutafuta usawa, jambo alilosema ni tofauti na Tanzania.
  •  
SHARE THIS STORY
Related Stories
“Mwaka 1991 nilipoteuliwa kuwa Mwanasheria Mkuu, niliulizwa ningetaka nini zaidi ambacho nitawafanyia Wakenya, nikajibu kuwa ningependa kuwa na Katiba mpya yenye kutoa haki na uhuru wa kweli kwa Wakenya,”  alisema.
Alisimulia kisa chake kwamba kutokana na ahadi hiyo, alikwenda Uswisi ambako alijifungia peke yake chumbani na kuandika Rasimu ya Katiba ndani ya siku 10, kisha akarejea Kenya na kuwaambia alichokifanya lakini akakataliwa na wengi akiwamo aliyekuwa Rais wa Kenya, Daniel Arap Moi.
Alisema mwaka 1995, Rais Moi alitangaza kuteua kamati ya wataalamu watakaoandaa upatikanaji wa Katiba na katika mchakato huo  walialikwa wataalamu watatu kutoka Ufaransa, Uganda na Zambia.
“Changamoto tuliyoipata kwa wakati huo ni kwamba, tuliambiwa kuwa tusiposhirikisha vyama vya kijamii na taasisi nyingine, wataweza kuipindua Serikali, hapo nataka kuonyesha namna gani makundi ya kijamii yalivyo ya muhimu zaidi,” aliongeza.
Hofu ya Kanu
Alisema kuwa Kanu bado iliendelea kuwa na hofu juu ya uchaguzi kutokana na jinsi mambo yalivyoanza kuwa motomoto baada ya tangazo la kuingia katika mfumo wa vyama vingi mwaka 1992, lakini tofauti na matazamio yao, Rais Moi aliibuka na ushindi mkubwa.
Baada ya hatua hiyo, alisema wanasiasa kutoka katika chama hicho kilichokuwa madarakani walisema hakukuwa na haja ya kuwa na Katiba mpya, bali wafanye maboresho kidogo kitendo kilichoibua hisia kali kutoka vyama vya upinzani.
Kingine ni Kanu kukataa kuingiza uwiano katika uchaguzi wa wabunge kwa madai ya wingi wao katika Bunge, jambo lililopingwa na wengi na kusababisha kuunda umoja uliojulikana kama Ufungamano.
Mwafaka katika Katiba
Kuhusu mwafaka alisema ulifika wakati ambao kila Mkenya aliona ipo haja ya kuwa na Katiba bila ya kujali maeneo wala mazingira anayotoka, ndipo wakakubaliana kukaa pamoja katika eneo la Boma na wakati huu walishiriki wabunge wote na wajumbe watatu kutoka kila wilaya na suala la mgawanyo wa majimbo likaibuka.
Rasimu yakataliwa
Pamoja na mambo yote, kosa lilikuwa jinsi walivyoipitisha kwa AG (yeye mwenyewe) ambapo alitakiwa kurekebisha katika maeneo 13, kisha akaipeleka bungeni, jambo lililoibua hasira za watu wakaamua kuipinga kwa makusudi.
“Huo ulikuwa ni mvutano wa kuonyeshana mabavu kwa wanasiasa na makundi mengine, kikubwa kilikuwa katika muundo wa majimbo na mgawanyo wa madaraka katika kuzalisha majimbo, ili kuwepo na seneta na gavana kabla ya wabunge,” alisema.
Anasema kuwa mamlaka zinatakiwa kuanzia ngazi ya mwanzo hadi katika ngazi ya Taifa likiwemo suala la kuangalia mgawanyo wa mapato ili kuondoa manung’uniko.
Ushauri Katiba ya Tanzania
“Katiba Mpya ambayo inatakiwa ni ile ambayo inaihusisha jamii moja kwa moja, tume yenu imefanya kazi nzuri na mpangilio uliofanywa na Rais kutanguliza maoni ya wananchi na kisha wao kuwa wa mwisho kuamua ni mpango mzuri ambao hata mimi nimeupenda,” alisema Wako. Alirudia maneno kuwa lazima maoni na matakwa ya wananchi yaangaliwe kwa umakini mkubwa kabla ya kuwarudishia ambapo watakwenda kuamua kwa busara bila ya malumbano.
Maswali ya wabunge
Mbunge wa Kongwa, Job Ndugai alimuuliza Wako kuhusu namna walivyokubaliana katika kugatua madaraka na njia bora ya kugawana rasilimali na katika majibu yake, Wako alisema kinachoweza kuondoa malalamiko hayo ni uamuzi wa wananchi katika Katiba ambayo inakwenda kutungwa itakayoeleza namna ya kugawana rasilimali za nchi kwa usawa.
Profesa Abdallah Safari aliuliza kwa nini Wako alitumia lugha ya Kiingereza katika hotuba yake, huku akijua kuwa Katiba ya Kenya katika ibara ya 8 imetamka wazi kuwa Kiswahili ndiyo lugha ya taifa hilo.
Wako aliomba radhi kuwa bado hajakijua Kiswahili vizuri kutokana na mazoea, na akasema alipochaguliwa alikwenda Zanzibar kujifunza Kiswahili kwa mwezi mmoja huku akiwataka watu kutumia lugha hiyo inayokuwa kwa kasi barani Afrika.