Subscribe:

Ads 468x60px

polisi wajeruhi watu 6 kwa mabomu wakiwa majumbani nyamongo


POLISI NYAMONGO WAJERUHI SITA KWA MABOMU WAKIWA MAJUMBANI KWAO.
Na Anthony Mayunga-Nyamongo.
Septemba 10,2012.

ASKARI  wa mkoa wa Kipolisi Tarime na Rorya wanadaiwa kujeruhi watu 6 wakazi wa kitongoji cha Nyabikondo kijiji cha Kewanja kwa kuwapiga mabomu wakiwa majumbani na kazini wakati wanawatanya  wavamizi wa kifusi cha mawe mgodini.

Tukio hilo limetokea septemba 9 ,majira ya saa 6 mchana mwaka huu katika kitongoji hicho,limethibitishwa na uongozi wa kitongoji na kijiji hicho,huku kamanda wa polisi mkoa akikwepa kulizungumzia kwa madai kuwa hakuwa na taarifa.

Ulipuaji mabomu na kuleta madhara kumetokea wakati taifa likizizima kuhusiana na mauaji yaliyofanywa na jeshi hilo kwa aliyekuwa mwakilishi wa Channel Ten mkoani Iringa Daud Mwangosi septemba 2 katika kijiji cha Nyololo wakati Chadema wanafungua matawi yao.

Waliojeruhiwa wametajwa kuwa ni Suzana Mwita Gibaye (28)ambaye aliumizwa kichwani na mguu wa kushoto,Ghati Marwa ambaye ni mjamzito ambaye habari zinadai kuwa amelazwa katika hospitali ya wilaya ya Tarime.

Wengine ni Esther  Chacha(12) Chacha Chacha(10) na Daniel Chacha(6) na mama yao Marwa Chacha ambao wamepanga kwa  Magaiwa Ngewa wanadaiwa  walipigwa  mabomu na kuumizwa wakiwa nyumbani kwao ambako anaendesha biashara ya mgahawa.
Majeruhi.

Mmoja wa majeruhi  Suzana akiongea na gazeti hili kwa njia ya simu  muda mfupi baada ya kutoka zahanati ya kampuni ya African Barrick North Mara kutibiwa alikopelekwa na askari polisi wa kituo cha Nyamomngo kuwa walipigwa wakiwa wanaendelea na kazi kwenye mgahawa wa Magaiwa.

“Tukiwa tunaendelea na kazi kwenye eneo la Mrwambe tuliona polisi wanafukuzana na vijana(Intruda) waliovamia kifusi kilichomwagwa nje na mgodi huku wanapiga mabomu ,lakwanza na la pili hayakutufikia wakapiga la tatu nikastukia napigwa kichwani na kitu na mguu wa kushoto damu zikaanza kuvuja nikaanguka huko”alisema.

Na kuwa mbali na yeye mama huyo na wanae wote wakawa wamejeruhiwa vibaya ,na polisi wakaendelea kupiga ovyo ovyo hali iliyopelekea kumwaumiza wananchi wengine wakiwa majumbani.

“Lilifika gari la pili la polisi afisa mmoja wakawachukua watoto na mama yao mimi nilikuwa nimeanguka kwa chini hawakuniona ,wakawapeleka zahanati ya mgodi ,mimi nilichukuliwa na boda hadi hospitali ya Sungusungu wakaniambia niwape Pf 3,kurudi polisi wakanipeleka zahanati ya mgodi”alidai.

Na alifungwa bendeji kichwani na mguuni na dawa kisha akarudishwa polisi na kusaini maelezo na kuambiwa arudi nyumbani akizidiwa arudi polisi,maelezo ambayo pia walipewa mama na watoto wake.

Mwenyekiti wa kitongoji.

Charles Vicent mwenyekiti wa kitongoji hicho alisema tukio hilo lilitokea wakati wakiwa kwenye kikao cha usuluhishi kati ya koo ya Nyabasi na Wanyamongo baada ya kutokea kutoelewana kilichohusisha Kamanda wa polisi wilaya aliyemtaja kwa jina la Saimoni,wazee na mila na viongozi wa maeneo husika.

“Tukiwa kwenye kikao mpakani mwa Kewanja na Nyakunguru ndipo pakatokea matukio hayo ambayo yalimlazimu Ocd kukimbilia eneo la tukio na kuwachukua wale watoto na mama yao na kuwapeleka mgodini wakafungiwa bendeji kisha wametelekezwa bila msaada wowote na inasemekana gololi ziliwaumiza kichwani na vifuani ”alisema.

Alidai kuwa askari polisi waliokuwa juu wakijua chini kuna makazi ya watu  walifyatua mabomu na kuelekeza majumbani na kuwa hili ni tukio la pili kupiga na kujeruhiwa watu wakiwa majumbani na shuleni.

Hata hivyo mama aliyejeruhiwa na wanae inasemekana baada ya kutoka zahanati ya mgodi kutibiwa inadaiwa aliondoka na wanae wala haijulikani alipo ,lakini habari kutoka kwa majilani zake zinadai kuwa huenda ameenda kwao kijiji cha Magoto kwa ajili ya matibabu zaidi na kuwa huenda walitishwa na polisi akaogopa.

Mwenyekiti wa serikali ya kijiji.
Akiongea na gazeti hili kwa njia ya simu Mwenyekiti wa serikali ya kijiji aliyejitambulisha kwa jina la Tanzania O’mtima alisema mmoja wa majeruhi ambaye ni mjamzito ambaye alipigwa akiwa nyumbani kwake inasemekana amepelekwa hospitali ya wilaya ya Tarime kwa matibabu zaidi.

Maelezo yake yanadhihirishwa na juhudi za baadhi ya mashuhuda walioongea na gazeti hili ,ambao walikwenda hospitali ya Sungusungu na hawakumkuta na hata walipofuatilia nyumbani kwake waliambiwa toka alipochukuliwa siku ya tukio hajarudi nyumbani.

Mgodi.
Mmoja wa maafisa wa mahusiano wa kampuni ya African Barrick North Mara Shayo Simion alipotakiwa kutoa ufafanuzi wa watu wanaohudumiwa na zahanati yao,alidai ni kwa ajili ya watumishi.

“Kama tumekuta mtu ameumia sisi hutoa msaada wa matibabu lakini kwa ajili ya majeruhi kama hao wanapaswa kupelekwa hospitali ya serikali,hilo wasiliana na kamanda kwa kuwa halituhusu”alisema.

RPC.
Kamanda wa mkoa huo wa kipolisi Justus Kamugisha alipoulizwa kuhusiana na kujeruhi watu kwa mabomu wakiwa majumbani alidai hakuwa na taarifa ya watu kuumizwa na mabomu ila vurugu za wananchi na askari.

“Vurugu ni kila siku tena leo wamepiga sana gari letu kwa mawe,hapajatokea utulivu eneo hilo ,maana watu wanajitokeza kwa wingi kutufanyia vurugu,hapa lazima maamzi magumu yachukuliwe ama kuondoa wananchi karibu na mgodi ama kampuni kutoka wachimbe kama zamani maana mgodi uko kwenye makazi ya watu ni hatari zaidi”alisema kamanda.

Baadhi ya mashuhuda wanadai kuwa wananchi walilazimika kushambulia magari ya polisi kwa kile walichodai matumizi ya nguvu ni makubwa ambayo yanasababisha madhara hata kwa wasiohusika.

Juhudi za kujua hali ya Ghati ambaye ni mjamzito alikolazwa na hali yake  zinaendelea baada ya kuwepo na usiri mkubwa ,ikizingatiwa kuwa hata majeruhi walipelekwa na polisi kutibiwa mgodini badala ya hospitali ya serikali ili kuficha taarifa.

Mwisho.



0 comments:

Post a Comment