Subscribe:

Ads 468x60px

Kijazi awapa somo wabeba mizigo Kilimanjaro



  


na Grace Macha, Moshi

   





MKURUGENZI Mkuu wa Hifadhi za Taifa nchini, (TANAPA), Allan Kijazi, amewataka wapagazi wanaosaidia kubeba mizigo ya watalii kwenye  Mlima Kilimanjaro kuhakikisha wanatunza mazingira ya mlima huo kwani ukiharibika na wao wataathirika kwa kukosa ajira.
 Aidha, alisema atawasiliana na wadau wa utalii ili kuona namna ya kuboresha utendaji wao kwa kuwatafutia ziara ya mafunzo kwenye moja ya nchi zenye milima mirefu.
 Aliyasema hayo jana wakati akifungua kongamano la kwanza la Chama Cha Wapagazi nchini (TPO) lililofanyika kwenye ukumbi wa YMCA ambalo lilikuwa likijadili changamoto wanazokabiliana nazo na namna ya kuzitatua.
 Kijazi alisema kuwa kwenye kongamano lao hilo mbali ya kujadili changamoto zinazowakabili ni vema wakaangalia namna ya kuutunza mlima huo ambao unawapatia ajira.
 “Kuna malalamiko yanakuja kuwa wakati mwingine nyie mnaacha taka huko mlimani kwa kushindwa kuzikusanya vizuri, ni vema mkautunza mlima huu kwani ukipoteza sifa na hadhi yake wageni wataacha kuja na nyie mtakosa ajira,” alisisitiza mkurugenzi mkuu huyo wa Tanapa.
Aliwataka viongozi wa TPO kujenga mfumo wa kufuatilia mienendo ya wanachama wao ili kuona kama wanafuata taratibu na maadili waliyojiwekea, kwani kuna wakati yanaibuka malalamiko kuwa kuna baadhi ya wapagazi si waaminifu na wengine hawazingatii uvaaji sahihi, jambo linalohatarisha usalama wa afya zao.
 Kijazi alisema kuwa anaangalia uwezekano wa kukutana na wadau wa utalii wanaoendesha shughuli kwenye mlima huo wakiwemo Chama cha Waongoza Watalii kwenye mlima huo, KIATO, na Wizara ya Maliasili na Utalii ili waweze kuona namna sheria zilizowekwa hasa kwenye udhibiti wa uzito wa mizigo zitakavyosimamiwa kwa ukaribu zaidi.
 Kwa upande wa Mwenyekiti wa Bodi ya Ushauri, TPO, Richard Kessy, alisema changamoto kubwa zinazowakabili wapagazi ni kampuni za uwakala wa utalii  kubebeshwa mizigo mizito zaidi ya kiwango kilichowekwa na Hifadhi ya Mlima Kilimanjaro (KINAPA) ambacho ni kilogramu 20.
 “Wapagazi wakiwa huko mlimani kuna wengine wanapewa chakula mara moja kwa siku, wengine wanapewa mara mbili lakini kidogo sana ukinganisha na kazi ngumu ya kubeba mizigo yao na ya watalii wanayoifanya,” alisema Kessy.
 Naye Mwenyekiti wa TPO, Philip Mbise, alisema kuwa wana wanachama 2,820, ambapo kongamano hilo la siku moja limehudhuriwa na wapagazi 250 kutoka mikoa ya Kilimanjaro na Arusha.