Subscribe:

Ads 468x60px

mtoto abeba majukumu ya wazazi




 Juma na mdogo wake Danieli wakiwa wodini











MTOTO ABEBA MAJUKUMU YA FAMILIA

Na Anthony Mayunga
Oktoba 6,2012.

“NILIISHIA darasa la tatu….wadogo zangu wote hawajaanza shule na sijui kama wataanza ….maana mimi ndiye nimegeuka mzazi wao…kula kwao ni mimi…wakigua kama huyu mimi ndio wananitegemea ndiyo maana leo niko wodini nikiuguza mdogo wangu,”ni maneno yaliyojaa simanzi ya mtoto Juma Deus(12)

Katika mazingira ya kawaida huwezi kuamini lakini ndivyo alivyokutwa na Mwandishi wa makala hii wodi ya watoto kitanda namba 1 hospitali teule ya Nyerere ddh wilayani Serengeti  mtoto  Juma akimuuguza mdogo wake Daniel Deus(5)akisumbuliwa na malaria na kuishiwa damu.

Anasema alilazimika kutembea kilometa zaidi ya 25 kwa mguu akiwa amembeba mdogo wake  mgongoni kutoka kijiji cha Nyakitono ambako baba yao Deus Marwa aliwaacha na kwenda kijiji cha Rung’abure baada ya kutoka hospitali alikokuwa amelazwa na kufanyiwa upasuaji wa tumbo septemba 3 mwaka huu.

Ilikuwaje?
Anasema septemba 20 majira ya saa 10:00 alfajiri mwaka huu bila kujali giza alilazimika kumbeba mdogo wake baada ya kuzidiwa na kuanza kutembea huku wakipumzika njiani na kila akipata nguvu aliendelea na safari.

“Sijui kama watoto wengine wanapata shida kama zangu,mdogo wangu hakuwa na uwezo wa kutembea nililazimika kumbeba mgongoni na kila nilipochoka tulikaa chini ,njaa ,uchovu viliniandama ,lakini kila nikikumbuka kama kuwa anahitaji tiba nilipata nguvu na kuanza safari”anasema huku akilengwa lengwa na machozi.

Anadai alitumia masaa zaidi ya 11 kufika kijiji cha Rung’abure aliko baba yake na kaka yao ambaye ni mtoto wa baba yao mwingine ambaye ni fundi baiskeli aliyemtaja kwa majina ya Mwita Deus.

“Tulifika tumechoka sana ,njaa na mdogo wangu kutokana na njaa na ugonjwa hali ilikuwa mbaya,tulimkuta baba akiwa naye hajapata nafuu ,tukakaa hapo kwa kaka tukawa tunamnunulia dawa mdogo wangu hali ikawa inazidi kuwa mbaya kila kukicha”anabainisha.

Septemba 27,mwaka huu akalazimika kuanza safari ya kumpeleka mdogo wake hospitali ya Nyerere ddh kwa kumbeba mgongoni hadi alipopata msaada kutoka kwa msamaria mwema.

Mtoto huyo ambaye kutokana na majukumu ya kulea wadogo zake amelazimika kuwa kama mtu mzima anadai  alianza safari hiyo lakini akapata msaada kutoka kwa kaimu afisa mtendaji wa kijiji cha Rung’abure Mkeba Mweri Masiko akawabeba kwa pikipiki hasa baada ya kumsimulia kilichowakuta.

“Kwa kweli msaada wake sitausahau kwa kuwa aligeuka kuwa mzazi wetu ,maana hakuishia kutusafirisha tu bali ameendelea kutusaidia,mpaka sasa ,maana kwa hali aliyokuwa nayo mdogo wangu tulipofika tu tukalazwa”anadai.

Juma anafafanua kuwa alikuwa na siku chache tu toka ametoka hospitalini hapo alipokuwa akimuuguza mdogo wake Wantiko Deus(4)”nimefika nyumbani namkuta huyu naye ana hali mbaya nimekuja hapa tumelazwa tena ,safari zote mpaka tunatoka hakuna ndugu anakuja kutuona tunasaidiwa na wagonjwa na ndugu zao wodini,maisha gani haya jamani”anasema kwa masikitiko.

Licha ya kuwa ni mtoto wa mama yake wa kambo lakini kwa vile kwao ndiyo mkubwa analazimika kuwasaidia wadogo zake bila ubaguzi wowote.

Fedha walizopewa kidogo zilitumika  kwa kununua dawa licha ya kuwa alitakiwa kutibiwa bure kulingana na umri wake lakini aliambiwa hakuna dawa ,hata hivyo hospitali hiyo inakabiliwa na upungufu wa dawa kutokana na kuwa toka Mei hawajapata dawa MSD kwa madai serikali haijatoa fedha za ruzuku.

Fedha hizo pia zilitumika kwa ajili ya kununulia chakula na zilipokwisha kwa kuwa wamekaa zaidi ya siku tano huku mdogo wake akitakiwa kula vyakula vizuri na matunda kwa kuwa alikuwa ana upungufu wa damu ikabidi ategemee msaada wa wagonjwa wenzake.

Maisha yao yalivyokuwa awali.

Mwaka 2009 walikuwa wakiishi katika kijiji cha Mbalibali baba yao akiwa na wanawake wawili,kisha akahamia kijiji cha Nyakitono yeye akiwa darasa la tatu walipofika huko hakupelekwa shule kwa madai kuwa baba yake hana uwezo na baadae mama zao wote wakakimbia na kuwaacha wao na baba yao.

“Mama yangu Pili Budaga aliondoka na kwenda kwao Usukumani na mama mdogo Pili Nyamhanga yuko kijiji cha Bonchugu hao wote waliondoka baada ya kukorofishana na baba ,wakaniachia mzigo huo najuta kuzaliwa mkubwa maana baba hajali familia yake”anasema kwa uchungu.

Kutojali huko ndiyo maana hajapelekwa  shule yeye  na hata  wadogo zake waliotakiwa kuanza shule ama darasa la awali hawajapelekwa,madai ya baba yao yakiwa ni kwamba hana uwezo.

Kutokana na hali ya kifamilia kuwa ngumu baba yao naye akawa hajali matokeo yake yeye akawa analazimika kubeba majukumu ya kuwahudumia wadogo zake kwa mahitaji ya chakula na kuchunga mbuzi walionao.

“Sijui hali ilivyo nyumbani kwa wadogo zangu kwa sasa wakati mimi niko huku ,wanapataje chakula ,tuna mbuzi 14 nani anawaangalia kwa kweli naumia sana ,sijui hali yao maana Nyamhanga ndiye mkubwa miaka 10,Wantiko(4)na Rhobi(3)ambao ndio wanaangalia mji”anasema kwa unyonge.

Muuguzi wa zamu.

Nyamtondo Masini muuguzi wa zamu wodi la watoto anakiri kuwa hali ya mtoto huyo haikuwa nzuri kwa sababu walimchelewesha kumfikisha hospitali kwa ajili ya matibabu.

“Mara ya pili mtoto huyu anakuja na wadogo zake kuwauguza,kwa kweli hili tukio si la kawaida hata kama baba yake hana uwezo lakini inatakiwa ndugu wasaidie kwa kipind chote anayeonekana ni mtu aliyewaleta hapa kwa pikipiki baada ya kuwakuta njiani “ anasema.

Shuhuda anena.
Magreth Samweli(32)mkazi wa kijiji cha Bonchugu ambaye mwanae amelazwa wodi hiyo anasema kwa mara ya kwanza anashuhudia mtoto anauguza mtoto mwenzake bila hata wazazi ama ndugu kuonekana.

“Huyu mtoto katembea umbali mrefu akiwa amembeba mdogo wake hadi sasa amefika hospitali hakuna ndugu anakuja kuwaona badala yake wanaouguza watoto wao humu ndiyo tumegeuka kuwasaidia “anasema.

Anakichukulia kitendo hicho kuwa ni cha kinyama na kinakiuka sheria na haki za mtoto kwa kuwa anastahili kutibiwa na kuhudumiwa na wazazi wake ama ndugu na kutaka serikali iwachukulie hatua kwa mzazi wake kwa kuwa kitendo cha kuoa wanawake wengi wakati hana uwezo wa kuwatunza watoto.

Kaimu ofisa mtendaji.

Mkeba Mweri Masiko kaimu ofisa mtendaji wa kijiji cha Rung’abure anasema baada ya kuwasaidia usafiri hadi hospitali amelazimika kubeba majukumu ya kuwahudumia baada ya kubaini kuwa hawakuwa na msaada wowote kutoka kwa ndugu.

“Hata damu nililazimika kutoa mimi baada ya kuona mtoto huyo anaweza kupoteza maisha,nimegeuka kuwa mzazi wao maana ninavyozungumza na wewe nimewatoa hospitali wako nyumbani kwangu nategemea kaka yao akifika niweze kumkabidhi hao wadogo zake,”anasema.

Kaka yake.
Mwita Bhoke ndugu yao na hao watoto anakiri watoto hao walitembea hadi kijiji hapo wakitafuta msaada baada ya baba yao kuwaacha na kwenda kupumzika kwake kutokana na ugonjwa aliokuwa nao.

“Niliondoka kwenda kijiji cha Mikomarilo Bunda kumwona mgonjwa mtoto huyo akazidiwa ndipo wakampeleka hospitali,kwa kweli hawakuwa na msaada wowote walijiuguza wenyewe baba yao alikuwa hapa hana kitu,alichofanya ni kutoka na kwenda kwenda kijiji cha Bonchugu kumsaka mkewe ambaye ni mama wa watoto hao maana walikuwa wamekosana”anasema.

Anasema watoto hao wako nyumbani kwake”hata wale waliobaki kijijini Nyakitono wamekuja huku kwa mguu nan i wadogo kutokana na kukosa huduma,hapa ninao watoto watatu, Juma ambaye ni mkubwa ameondoka na wazazi wake kwenda Nyakitono kuangalia mji.”amebainisha.

Akizungumzia uhusiano wao alidai hao ni watoto wa baba yao mdogo na maisha ya baba yao yamekosa msimamo kwa kuwa anavurugana na wake zake matokeo yake watoto ndio wana hangaika kama ilivyo sasa na hata shule imeshindikana.

Matatizo ya watoto yarudisha mahusiano ya wazazi.

Bhoke anafafanua kuwa matatizo hayo yameweza kurudisha mahusiano ya wazazi kwa kuwa mke wake amerudi ili waweze kusaidiana kulea watoto ambao wanaleana wao kwa wao huku Juma akilazimika kubeba majukumu mazito.

Mwenyekiti wa serikali naye avunja kimya.
Mwenyekiti wa serikali ya kijiji cha Rung’abure Charles Kibure akiongea na Mwananchi Jumapili amesema taarifa za watoto hao alizipata kupitia kwa kaimu afisa mtendaji na kumsaka Bhoke,hivyo anataraji kumbana mzazi wa watoto hao ahakikishe anawahudumia.

Kijijini kwake hawana  taarifa.

Mwenyekiti wa serikali ya kijiji cha Nyakitono Juma Porini anasema hana taarifa za familia hiyo ,”huyo Deus Marwa simjui maana kama kulikuwa na tatizo hilo ,hata hivyo hapa kijijini tunasaidia wale wasiokuwa na uwezo kabisa kwa matibabu na hata elimu ,ngoja nafuatilia”anasema.

Wanaharakati.

Baadhi ya wanaharakati wanasema matukio kama hayo yanachangiwa na wazazi wengi wanaooa wake wengi kutothamini familia zao na hata kushindwa kuwapeleka shule,lakini hakuna hatua ambazo wanachukuliwa .

Juhudi za kuwasaka wazazi hao ili kujua hatima ya watoto hao kwa masuala ya elimu.
Mwisho.0759891849.









0 comments:

Post a Comment