Subscribe:

Ads 468x60px

Ngariba anaswa baada ya kukeketa watoto wawili

NGARIBA ANASWA BAADA YA KUWAKEKETA WATOTO WAWILI.
Na Anthony Mayunga-Musoma
Novemba 15,2012.

NGARIBA na mmoja wa wazazi wakazi wa kijiji cha Masurura kata ya Bwiregi wilaya ya Butiama wanashikiliwa na jeshi la polisi mkoa wa Mara kwa tuhuma za kuwakeketa watoto wawili wa kike ambao ni wanafunzi wa shule ya msingi Masurura.

Kukamatwa kwa watuhumiwa hao novemba 10 mwaka huu  kunakuja huku maeneo mengi maandalizi ya kuwakeketa watoto wa kike yanaendelea  ,wakisubiri shule za msingi zikifungwa.

Kamanda wa polisi mkoa wa Mara Absalom Mwakyoma amewataja walikamatwa kuwa ni ngariba Bhoke Wambura(60)mkazi wa kijijini hapo ambaye anadaiwa kuwakeketa watoto wawili na mmoja kufanikiwa kukimbia na kujisalimisha polisi.

Amesema ngariba huyo alilipwa tsh,5,000 na kuwakeketa watoto wawili ambao majina yake yamehifadhiwa na ikiwa ni kinyume na sheria ya makosa ya kujamiiana ya mwaka 1998 na  sheria ya Mtoto ya mwaka 2009.

“Pamoja na ngariba tumemkamata mama ya mmoja wa watoto waliokeketwa Ghati Mwita(48)wote wa kijijini hapo ,tunawashikilia na tutawafikisha mahakamani kwa kosa hilo wakati wowote”alisema.

Kamanda huyo alisema mtoto aliyetoroka kwa kukwepa kukeketwa na kujisalimisha polisi wamemhifadhi kituo cha polisi Musoma wakiendelea kuwasaka wote waliohusika katika mpango huo unakiuka sheria na Haki za Binadamu.

Kutokana na maandalizi yanavyoshika kasi tayari ameelekeza nguvu katika kata za Ryamisanga,Wegero na Kamugendi kwa wilaya ya Butiama ambako inadaiwa kuwepo maandalizi ya ukeketaji.

“Nimeishatoa maelekezo kwa kila kamanda wa polisi wa wilaya kuhakikisha maeneo yote yanayodaiwa kuwepo maandalizi yafuatiliwe ili watakaohusika wakamatwe kwa kuwa hatuwezi kuona sheria zinavunjwa ,maana hayo ni makosa ya jinai”alisisitiza kamanda.

Hivi karibuni mkuu wa mkoa wa Mara John Tupa akiongea naBlogu hii  kwa njia ya simu kuhusiana na mikakati ya mkoa kukabiliana na ukeketaji alisema viongozi wote kuanzia ngazi za vitongoji ,wazee wa mila wameishaelezwa msimamo wa serikali.

Alisema atakayekaidi atakamatwa na kushitakiwa kwa mjibu wa sheria na kuwaomba wazazi na walezi kuhakikisha wanatii bila shuruti kwa kuwa hawatasita kuwafikisha mahakamani.

Shirika la  Chidren’s Dignity Forum(CDF) lililoko wilayani Tarime likizindua ripoti ya utafiti lilisema kuwa watoto 4,000 wilayani Tarime wako hatarini kukeketwa.

Pamoja na msimamo wa serikali kumebainika kuwepo mbinu mbalimbali zinazoandaliwa na wazee wa mila kuhakikisha watoto wa kike wanakeketwa ikiwemo kazi hiyo huenda ikafanyika usiku,kwa walio mipakani kupelekwa nchi Kenya kwa ajili ya kukeketwa .

Pia baadhi ya vijana kutishia kugoma kutahiriwa iwapo wasichana hawatakeketwa kwa kuwa hukaa jandoni wote na hutoka siku moja,msukumo ambao unawapelekea wazee wa mila kuhaha kuhakikisha ukeketaji unafanyika ili kulinda mila na desturi.

Mwisho.


0 comments:

Post a Comment