Subscribe:

Ads 468x60px

Kisumo amtaka Kikwete kuwaiga waliomtangulia


Na Daniel Mjema, Mwananchi

Posted  Jumatatu,Decemba23  2013  saa 9:29 AM
Kwa ufupi
  • “Kwangu mimi sifa kubwa zaidi ni kwa Kinana... itakuwa upuuzi chama kinachotawala kikaacha haki yake ya kuwatetea wanyonge kwa kupima utendaji wa wale kiliowapa dhamana ya uongozi,” Kisumo
Moshi. Mwanasiasa mkongwe, Peter Kisumo amesema kuna tatizo katika uchujaji (vetting) wa watu wanaoteuliwa kushika madaraka ya umma wakiwamo mawaziri na kutaka mfumo huo urekebishwe.

Pia Kisumo alisema Rais Jakaya Kikwete anapaswa kuiga mfano wa marais waliomtangulia kwa kuchukua hatua za kuwaondoa mawaziri wanaochafua taswira ya nchi badala ya kusubiri Bunge.

Akizungumza jana, Kisumo alisema ni lazima uchujaji wa watu wanaoteuliwa kuwa mawaziri na watumishi wengine wa ngazi za juu uzingatie uadilifu na siyo mapenzi ya Rais pekee.

Kisumo alikuwa akizungumzia hatua ya Rais Jakaya Kikwete kutengua uteuzi wa mawaziri wanne iliyotangazwa na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda baada ya shinikizo kubwa kutoka kwa wabunge.

Kisumo alisema ni lazima vyombo vya kumshauri Rais vifanye kazi yake kwa masilahi ya nchi vinginevyo Watanzania wataendelea kushuhudia mawaziri waking’oka kwa kushindwa kuwajibika.

Alitolea mfano kuwa  Rais wa Kwanza Mwalimu Julius Nyerere, aliwahi kumteua Chediel Mgonja (marehemu) kuwa Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga lakini akamwondoa kabla ya kumwidhinisha.

Kisumo alisema wakati wa Nyerere na hata awamu ya Benjamin Mkapa (1995-2005), wapo mawaziri waliowajibishwa na Rais lakini awamu zote mbili za Rais Kikwete mambo yako tofauti.

“Wakati wa Nyerere akipata taarifa kuwa taswira ya nchi inaharibika alikuwa anawaita na kuwataka wamuandikie barua ya kujiuzulu lakini awamu zote hizi za Kikwete mambo yanaanzia bungeni,” alisema na kuongeza:

“Kusubiri hadi upate shinikizo la Bunge wakati una uwezo wa kuwaondoa watu wako mapema haipendezi sana… haya nayaona awamu ya Kikwete.”

Mwanasiasa huyo alimpongeza Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana kwa kufanya kazi ya kutathmini utendaji wa Serikali akisema hajawahi kupatikana katibu mkuu wa aina yake tangu 1995.

“Kwangu mimi sifa kubwa zaidi ni kwa Kinana... itakuwa upuuzi chama kinachotawala kikaacha haki yake ya kuwatetea wanyonge kwa kupima utendaji wa wale kiliowapa dhamana ya uongozi,” alisema.