Subscribe:

Ads 468x60px

Uhaba wa madarasa wakosesha Wanafunzi 16,482 kuingia sekondari


Posted  Decemba28  2013  saa 9:28 AM

 Na Goodluck Eliona, Mwananchi
Kwa ufupi
  • Wanafunzi hao ni kati ya 844,938 waliofanya mtihani wa darasa la saba Septemba 11 na 12, 20013, ambapo 427,609 walifaulu kwa kupata alama A na C, ambayo ni sawa na asilimia 50.61 ya ufaulu.
Dar es Salaam. Serikali imetangaza idadi ya wanafunzi waliochaguliwa kujiunga kidato cha kwanza mwakani, huku 16,482 wakishindwa kuchaguliwa kutokana na uhaba wa madarasa.
Wanafunzi hao ni kati ya 844,938 waliofanya mtihani wa darasa la saba Septemba 11 na 12, 20013, ambapo 427,609 walifaulu kwa kupata alama A na C, ambayo ni sawa na asilimia 50.61 ya ufaulu ikiwa ni ongezeko la asilimia 19 ikilinganishwa na matokeo ya mwaka jana.
Akitangaza matokeo hayo jijini Dar es Salaam jana, Katibu Mkuu wa Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Jumanne Sagini alisema jumla ya wanafunzi 867,983 walisajiliwa kufanya mtihani huo, lakini wanafunzi 23,045 hawakufanya kutokana na utoro, vifo na ugonjwa.
Alisema kuwa kutokana na ongezeko la fursa ya utoaji wa elimu ya sekondari nchini, wanafunzi 411,127 kati ya 427,609 waliofaulu mtihani wamechaguliwa kujiunga na kidato cha kwanza katika shule za serikali awamu ya kwanza huku zaidi ya 16,000 wakikosa kuchaguliwa kutokana na uhaba wa vyumba vya madarasa 412.
“Idadi hiyo ni sawa na asilimia 96.15 ya wanafunzi waliofaulu mtihani. Kati ya wanafunzi hao wasichana ni 201,021 sawa na asilimia 95.9 na wavulana ni 210,106 sawa na asilimia 96.3,” alisema Sagini na kuongeza kuwa:
“Ninaziagiza Halmashauri zilizobaki katika awamu ya kwanza ya uchaguzi kukamilisha ujenzi wa vyumba vya madarasa ili kuwawezesha wanafunzi kujiunga na kidato cha kwanza ifikapo Machi 2013.”
Katibu Mkuu huyo aliongeza kuwa ikilinganishwa na matokeo ya mwaka jana, idadi ya wanafunzi waliochaguliwa kuingia kidato cha kwanza imeongozeka kwa asilimia 31.37.
Alisema kuwa mtihani huo ambao ulifanyika Septemba 11 na 12, mwaka huu, ulisahihishwa kwa kutumia teknolojia ya kompyuta ‘Optical Mark Reader (OMR)’.
“Mwanafunzi aliyepata alama ya juu kabisa kwa upande wa wavulana alipata 244 kati ya 250 huku msichana akipata 241. Mwaka 2012 alama ya juu ilikuwa 237,” alisema.
Akizungumzia vitendo vya udanganyifu kwenye mtihani huo, Sagini alibainisha kuwa wanafunzi 13 wamefutiwa matokeo yao, ambayo ni idadi ndogo ikilinganishwa na watahiniwa 219 waliofutiwa matokeo mwaka 2012.
“Napenda kutoa wito kwa walimu, wazazi na jamii kwa ujumla kujiepusha na vitendo vya udanganyifu kwani vinatoa taswira mbaya kwa taifa na kuwafanya watoto wetu wawe tegemezi zaidi kuliko kujituma na kujibidiisha katika masomo,” alisema.
Hata hivyo, Katibu Mkuu huyo hakutaja viwango vya ufaulu kwa kila somo kama ambavyo imezoeleka katika mitihani iliyotangulia wala mkoa uliofanya vizuri au vibaya. Matokeo ya mwaka huu yanaonyesha kuwa idadi ya wanafunzi walioshindwa kufanya mtihani imepungua kwa wanafunzi zaidi ya 6,000 ikilinganishwa na 29,012 ambao hawakufanya mtihani huo mwaka jana.

Huku idadi ya wasichana na wavulana walioshindwa kufanya mtihani ikipungua kutoka wasichana 12,501 mwaka jana hadi 9,781 mwaka huu na wavulana 16,511 hadi 13,264.
Matokeo hayo yameshindwa kufikiwa kwa malengo ya mpango wa Serikali wa Matokeo Makubwa Sasa (BRN) ambao uliwataka walimu kuhakikisha kuwa wanapandisha kiwango cha ufaulu hadi kufikia asilimia 60.
Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mkutano wa BRN kwenye sekta ya elimu jijini Dar es Salaam, Agosti mwaka huu, Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk Shukuru Kawambwa, alisema kuwa kiwango hicho cha ufaulu kilitakiwa kuanza kutumika mwaka huu. Aliwapongeza walimu, walimu wakuu, kamati za shule, waratibu wa Elimu Kata, Viongozi wa Halmashauri na wadau wote wa elimu ambao wanasimamia na kuendesha utoaji wa elimu nchini.
Akisoma hotuba ya Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi, bungeni Dodoma mwaka huu, Dk Kawambwa alisema kuwa serikali itafanya ufuatialiaji wa namna ya uendeshaji wa mitihani ya darasa la nne, mtihani wa kumaliza elimu ya msingi.
Mitihani mingine aliitaja kuwa ni wa ufundi stadi katika Halmashauri tisa ambazo ni Temeke, Ilala, Kinondoni, Morogoro Mjini, Morogoro Vijijini, Kibaha Mjini, Kibaha Vijijini, Bagamoyo na Kisarawe, ili kubaini wanafunzi wenye matatizo katika ujifunzaji.