Subscribe:

Ads 468x60px

Mapigano yaua wakulima wanne


23/12/2013 | Posted by Danson Kaijage |  

MGOGORO kati ya wakulima na wafugaji wilayani Kiteto, Manyara umeingia sura mpya baada ya wafugaji wa jamii ya Kimasai kuwavamia wakulima na kusababisha vifo vya watu wanne.
Taarifa ya Mkuu wa Polisi Mkoa wa Manyara, Akilimali Mpwapwa, ilieleza kati ya watu hao, watatu walikufa hapo hapo na mmoja akiwa njiani kupelekwa hospitali ya rufaa ya Mkoa wa Dodoma na majeruhi saba.
Alisema usiku wa kuamkia Jumamosi, wafugaji waliingiza mifugo yao katika mashamba ya wakulima katika eneo la Kijiji cha Olupoponyi, Kitongoji cha Kalakala.
Alisema kitendo hicho ndicho kilichosababisha wakulima nao kuanza kuwazuia wafugaji na mifugo yao kutolisha mimea yao, lakini baada ya hapo wafugaji walionekana kuwa wabishi na kuanza kuwashambulia.
“Kutokana na majibishano kati ya wafugaji na wakulima ilisababisha wakulima watatu kupoteza maisha na majeruhi saba ambao walilazwa katika hospitali ya Wilaya ya Kiteto,” alisema.
Mauaji hayo yalitokea Kijiji cha Olupoponyi, Kitongoji cha Kalakala ambapo Mbunge wa Kiteto na Naibu Waziri wa Mifugo na Maendeleo ya Uvuvi, Benedict Ole-Nangoro (CCM) anaishi.
Imeelezwa jamii ya wafugaji wa Kimasai waliwavamia wakulima wakiwa katika vibanda vyao wamelala, saa 7 usiku na kuanza kuwashambulia kwa mapanga, sime, mikuki, visu na risasi.
Mbunge wa Kongwa na Naibu Spika wa Bunge, Job Ndugai, alisema kitendo ambacho kinafanywa na wafugaji dhidi ya wakulima ni cha kinyama zaidi.
Hata hivyo, alieleza kushangazwa na serikali kufumbia macho mgogoro huo ambao kimsingi ni wa miaka mingi.
“Wafugaji wa jamii ya Kimasai wamekuwa wakiwaua wakulima mara kwa mara na wala suala hili si geni, viongozi wa ngazi ya juu wamekuwa wakiambiwa masuala haya, lakini kinachoshangaza ni kuona ukimya wa viongozi,” alisema.
Mbali na hilo, alimshambulia mbunge wa Kiteto, Ole-Nangoro kuwa ni kati ya viongozi wanaochochea chuki na kukuza ukabila katika Wilaya ya Kiteto.
Hivi karibuni, Ndugai alifanya mkutano na wakulima katika mji mdogo wa Kibaigwa, wilayani Kongwa na kuwaeleza kuwa Wilaya ya Kiteto kwa sasa imechafuka kutokana na viongozi wake kuwa na tabia ya kuendekeza ukabila.
Mbali na kuwepo na vitendo vya ukabila na ubaguzi, aliwataja Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Dk. Rehema Nchimbi na Mkuu wa Mkoa wa Manyara,  Elaston Mbwilo kuwa wanahusika kwa kiasi kikubwa kuchochea mgogoro kutokana na kupokea rushwa kutoka kwa wafugaji.