Subscribe:

Ads 468x60px

Mikoani washangilia mawaziri kung’oka


Na Waandishi Wetu, Mwananchi

Posted  Jumatatu,Decemba23  2013  saa 9:33 AM
Kwa ufupi
  • Diwani wa Nyanungu, wilayani Tarime Mkoa wa Mara, Samson Mang’enyi alisema operesheni hiyo ilifanywa kwa uonevu na kuwaathiri wananchi wanaoishi pembezoni mwa Hifadhi ya Serengeti.
Mikoani: Wananchi katika mikoa mbalimbali nchini wameshangilia kung’olewa kwa mawaziri wanne, yakiwa ni matokeo ya uchunguzi wa Bunge kuhusu Operesheni Tokomeza Ujangili.

Diwani wa Nyanungu, wilayani Tarime Mkoa wa Mara, Samson Mang’enyi alisema operesheni hiyo ilifanywa kwa uonevu na kuwaathiri wananchi wanaoishi pembezoni mwa Hifadhi ya Serengeti.
Mang’enyi alidai kuwa askari wa wanyama pori wamekuwa wakiwapiga risasi raia na mifugo na kwamba wakati mwingine wamekuwa wakiwafanyia vitendo vya kinyama kina mama na watoto ambao walikuwa wakiingia katika Bonde la Nyanungu kuokota kuni.
“Miaka yote hapa kijijini tulikuwa tunategemea Bonde la Nyanungu katika kulishia mifugo yetu, kulima na kina mama na watoto kuokota kuni, lakini baada ya kutangazwa Operesheni Tokomeza, kwa kweli hii nchi haina ubinadamu kwa baadhi ya watu,” alisema diwani huyo.

Mkazi mwingine wa kata hiyo, Caro Chacha alisema afya yake kwa sasa inazidi kuzorota baada ya kuchapwa viboko visivyo na idadi na baadhi ya askari wanyama pori wa Hifadhi ya Serengeti (Senapa) alipokuwa akiokota kuni katika Bonde la Nyanungu.

“Kwa kweli kipigo nilichokipata sitakisahau katika maisha yangu. Nilikuwa nanyonyesha lakini nilishindwa hata kunyonyesha mtoto, hata namna ya kujisaidia haja ndogo nilishindwa. Ila Mungu ni mkubwa,” alisema na kuongeza:

“Askari hao walifikia hatua na kutuvua nguo zote, tukabakia uchi wa mnyama kama tulivyozaliwa, jamani inauma sana kwani pale walikuwapo watoto, walitufanyia vitendo vya ajabu sana. Walitaka hata kutubaka ila walishindwa baada ya kuona tumeishiwa nguvu kwa mateso ya muda mrefu.”

Ruvuma
Mkoani Ruvuma, wananchi wamekuwa na maoni yanayokinzana, baadhi wamepongeza uamuzi wa Bunge na baadaye Serikali, wakati wengine wameeleza kusikitishwa.

Mkazi wa Tunduru, Ajiri Omary Kalolo alisema anaunga mkono uamuzi wa mawaziri kuondolewa madarakani akisema naye ni mmoja wa watu walioteswa na askari waliohusika na Operesheni Tokomeza Ujangili.

Kalolo alisema mbali na mateso aliyopata, aliwekwa mahabusu, kunyang’anywa fedha na kushinda njaa.

“Ninaunga mkono kung’olewa mawaziri wenye dhamana. Hili ni funzo, kwani nchi ingekufumbua macho tatizo hili tungeweza kufika pabaya zaidi ingawa najua wapo askari ambao wametesa wananchi kwa matakwa yao na hawakutumwa kufanya hivyo, tunaiomba Serikali iwachukulie hatua zaidi,” alisema.
Mwenyekiti wa Chama cha Waandishi wa Habari Mkoa wa Ruvuma, Andrew Kuchonjoma ambaye pia alikamatwa na kuwekwa mahabusu kwa siku tatu kwa kosa la kukutwa na mbao, alielezea kusikitishwa kwake na  kung’olewa kwa mawaziri kwa makosa yaliyofanywa na watendaji waliopo chini yao.

Alisema hatua ya mawaziri kung’oka haitoshi badala yake akataka Serikali iwachukulie hatua askari wote waliofanya vitendo vya ukatili.
Morogoro
Katika Wilaya za Ulanga na Kilombero mkoani Morogoro, baadhi ya wananchi wameeleza kufurahishwa kwao na uamuzi wa Serikali wa kuwawajibisha mawaziri hao wakisema operesheni hiyo ilisababisha vifo vya watu na wanyama na kwamba hata walipolalamika hawakusikilizwa.
Mmoja wa watu aliyedai kwamba ndugu zake waliuawa katika operesheni hiyo, Hamis Kewala alisema suala la kumalizika kwa ujangili linahitaji umakini kwani wahusika walio wengi wamekuwa wakitumia mbinu mpya kuua tembo na kusafirisha meno hayo, huku wasiohusika wakiumizwa bila hatia.
Mkazi mwingine, Mohamed Nguku alisema: “Vita hii sasa itakosa nguvu, suala la msingi ni kuhakikisha usimamizi wa hali ya juu na umakini, halafu taratibu na sheria za nchi kwa wanaopewa dhamana kufanya kazi hizi lazima zifuatwe na siyo kufanya wanavyojua wao”.
Agosti 12 mwaka huu, Mkazi wa Tarafa ya Mwaya wilayani Ulanga, January Gunena alikamatwa na kupelekwa katika kambi ya mateso iliyokuwa katika Hifadhi ya Selous na  kuteswa na baadaye alifariki dunia.
Wengine waliopatwa na mateso hayo ni madereva wanaoendesha magari yanayofanya safari kati ya Ifakara, Mahenge na Mwaya ambao wakiwa safarini walikuwa wakisimamishwa na askari kuhojiwa lakini wengine wakiishia kupata vipigo na kuporwa fedha.
Imeandikwa na: Florence Focus (Tarime), Joyce Joliga (Songea), Lilian Lucas (Morogoro).