Subscribe:

Ads 468x60px

Pinda: Watumishi 866 wamechukuliwa hatua kwa ubadhirifu wa fedha


Na Jacqueline Massano
22nd December 2013

Waziri Mkuu, Mizengo Pinda
Watumishi 866 wa serikali wamechukuliwa hatua za kinidhamu na kisheria kwa ubadhirifu wa fedha katika halmashauri mbalimbali nchini.

Kauli hiyo ilitolewa jana bungeni na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda alipokuwa akisoma hotuba ya kuahirisha shughuli za Mkutano wa 14 wa Bunge lililofanyika mjini hapa.

Pinda alisema watumishi waliohusika na ubadhirifu wa mali na fedha za Umma wamechukuliwa hatua mbalimbali zikiwemo kusimamishwa kazi, kushushwa vyeo na kufikishwa mahakamani.

Aidha, alisema kesi za watumishi hao ziko katika mahakama na katika vyombo vya nidhamu vya Halmashauri na Tume ya Utumishi wa Umma kulingana na makosa yao.

Alisema kutokana na hali hiyo, kati ya mwaka 2011/12 hadi Septemba, mwaka huu jumla ya wakurugenzi 52, wakuu wa idara 65 na watumishi wengine 746 wamechukuliwa hatua za kinidhamu na kisheria kwa ubadhirifu wa fedha katika halmashauri mbalimbali nchini.

“Waliofukuzwa kazi ni 232, waliosimamishwa 186, waliovuliwa madaraka 33, waliopunguziwa mshahara 1, walioshushwa cheo 32, walipewa onyo 113, waliofikishwa mahakamani 233 na waliofikishwa polisi na Takukuru 36.

“Serikali itaendelea kuhimiza nidhamu katika matumizi ya kifedha na vilevile itaendelea kuchukua hatua dhidi ya watumishi wote watakaokuwa wabadhirifu,” alisema.

Aidha, alisema pamoja na hatua za kisheria zinazochukuliwa kwa watumishi hao mmoja mmoja, serikali imeendelea kuchukua hatua nyingine mbalimbali kukabiliana na tatizo la ubadhirifu wa mali za umma katika halmashauri.

Pinda alizitaja hatua za kukabiliana na ubadhirifu huo kuwa ni kuongeza uwezo kwa kuajiri wahasibu wa kutosha katika halmashauri, kuanzisha kamati za mapato na matumizi katika ngazi zote za halmashauri na kutoa mafunzo ya mara kwa mara kwa kamati za mapato na matumizi za halmashauri zote.

Alitaja mbinu nyingine zinazotumika ni kufanya ukaguzi maalum kubaini ufisadi na ubadhirifu wowote uliojitokeza.

“Kwa mfano katika mwaka wa fedha 2011/12 kumefanyika ukaguzi maalum kwenye Mamlaka za Serikali za Mitaa 14 ambazo ni Kilindi, Kiteto, Muheza, Ruangwa, Musoma, Kilwa, Temeke, Singida, Arusha, Mvomero, Morogoro, Dodoma, Mbarali na Bunda,” alisema.

Pinda aliahirisha Bunge hilo hadi Mei 6 mwakani katika mkutano wa 15 wa bajeti.
CHANZO: NIPASHE JUMAPILI